Benki ya Dunia imepongeza Serikali ya Tanzania kwa kutoa kipaumbele kwa sekta ya Elimu na kwamba ni moja kati ya nchi zilizofanikiwa sana katika kuhakikisha watoto wenye umri wa kwenda shule wanapata nafasi hiyo.
Pongezi hizo zimetolewa jijni dar es Salaam na Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Dunia ukanda wa nchi za Africa Anne Kabagambe alipofanya ziara katika shule ya Sekondari Kibasila akiwa na Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Joyce Ndalichako.
Mkurugenzi huyo ametembelea shule ya Kibasila kwa sababu Benki ya Dunia inaendelea kushirikiana na Serikali ya Tanzania katika juhudi zinazofanywa katika sekta ya elimu ikitambua kuwa elimu ni ndio chimbuko la maendeleo katika yoyote katika nchi.
Nae Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof Joyce Ndalichako amesema Benki ya Dunia imekuwa ikishirikiana na Serikali katika miradi mbalimbali ya maendeleo ikiwemo mradi wa Elimu unaojulika kama Lipa Kulingana na Matokeo (EP4R) ambapo Benki ya Dunia imetoa dola za kimarekani milioni 202 katika mradi huo ulioanza kutekelezwa mwaka 2014 na unategemewa kumalizika mwaka 2021.
Waziri Ndalichako amesema kupitia mradi huo takribani Sh bilioni 141 zimeshatumika kwa ajili ya kukarabati shule kongwe 62, kujenga vyumba vya madarasa 2,876, matundu ya vyoo 6,558, nyumba za walimu 59, mabwalo 76, majengo ya utawala 16, Mabweni 533 kwa ajili ya kuwaepusha watoto wa kike na changamoto za mbalimbali, pamoja na kujenga mifumo ya maji safi kwenye baadhi ya shule ambazo hazikuwa na vyanzo vya maji.
Aidha Waziri Ndalichako alisema kwa upande wa Shule ya Sekondari Kibasila Sh. shilingi milioni 900 zimetengwa kwenye bajeti ya mwaka wa fedha 2019/2020 kwa ajili ya ukarabati na tayari wataalamu wameanza kufanya tathmini ya majengo ya shule hiyo ambayo ukarabati wake utaanza wakati wowote kuanzia sasa.
Awali akitoa taarifa ya shule Mkuu wa Shule ya Sekondari Kibasila Yasinta Matilya amesema moja ya changamoto inayokabili shule hiyo ni utoro wa wanafunzi unaotokana na changamoto za kifamilia ikiwemo watoto kulelewa na mzazi mmoja, kipato duni, umbali wa makazi ya wanafunzi.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti wanafunzi wa shule hiyo wameiomba Serikali kuwapatia walimu wa saikolojia watakaowasaidia kujitambua ikiwa ni pamoja na kuwajengea mabweni ili kuepukana na vishawishi vya barabarani pamoja na usumbufu wa usafiri wa unaopelekea wanafunzi kuacha shule.
Share To:

msumbanews

Post A Comment: