Na Loretha Laurence-WHUSM,Dodoma
Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Dkt. Harrison Mwakyembe amempongeza mwanamitindo wa kimataifa Bibi. Flaviana Matata kwa juhudi za kusaidia watoto wa kike kupata elimu kwa kuwawezesha  vifaa muhimu vya shule ikiwemo ada na madaftari.

Akizungumza na waandishi wa habari jana Jijini Dodoma Dkt. Mwakyembe amewataka vijana wa kitanzania kuiga mfano wa mwanamitindo huyo ili kuchangia katika ujenzi wa taifa.

“Nawasihi vijana wengine wenye fursa kama za Flaviana Matata kuzitumia vizuri  kwa kuhakikisha jamii inanufaika na mafanikio waliyoyapata” ameongeza Dkt. Mwakyembe

Aidha, aliongeza kwa kueleza kuwa, Mwanamitindo huyo amekuwa ni balozi mzuri katika kupeperusha bendera ya Taifa katika nchi mbalimbali za Ulaya.

Kwa upande wake Naibu Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Mhe. Juliana Shonza amempongeza Bibi. Flaviana kwa kuwa  mfano bora kwa watoto wa kike kwa jinsi ambavyo amekuwa akisaidia watoto wa kike nchini.

Naye Mwanamitindo wa Kimataifa Bibi. Flaviana Matata ameleza kuwa mbali na kujishughulisha na mitindo, ameweza kuanzisha kampuni ya Flaviana Matata Foundation ambayo inasaidia kutoa vifaa vya shule, ambapo hadi sasa amefanikiwa kutoa vifaa zaidi ya 5000 katika shule mbalimbali nchini.

Anazidi   kueleza kuwa, Taasisi hiyo imefanikiwa kurabati shule mbalimbali kwa kujenga madarasa na  kusomesha wasichana 15 ambao wanamaliza kidato cha sita mwaka huu na wengine watano bado wapo shule.

Hata hivyo, Mwanamitindo huyo ameushukuru uongozi wa Wizara kwa jitihada za wazi wanazozifanya katika kusimamia haki za wasanii na hivyo kurudisha hadhi ya tasnia hiyo nchini.
Share To:

msumbanews

Post A Comment: