Na.Faustine Gimu Galafoni,Dodoma .
Wizara ya Elimu Sayansi na Teknolojia inatarajia kutenga Jumla ya Tsh.Bilioni 5.5 kwa ajili ya kufanikisha Mashindano ya Kitaifa ya Sayansi,Teknolojia na Ubunifu [MAKISATU]kwa mwaka wa fedha 2022/2023.
Hayo yamesemwa leo Mei,4,2022 na katibu Mkuu Wizara ya Elimu ,Sayansi na Teknolojia Prof.Eliamani Sedoyeka wakati akifungua mafunzo elekezi kwa Waandishi wa Habari mkoa wa Dodoma kuelekea wiki ya Ubunifu Tanzania.
Prof.Sedoyeka amesema wizara kupitia Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia [COSTECH]kwa kushirikiana na wadau mbalimbali zimejipanga kuhakikisha wabunifu kutoka makundi mbalimbali wanaibuliwa.
“Wizara imeendelea Zaidi kujipanga katika kuhakikisha wabunifu wanaibuliwa ,kwa mwaka huu ,Zaidi ya Tsh.bilioni 1 zimetengwa na kwa mwaka ujao wa fedha 2022/2023 matarajio ni kutenga Tsh.Bilioni 5.5 hivyo ninyi wadau wa habari ni wadau muhimu wa kuibua kutangaza na kuibua wabunifu”amesema.
Aidha,Prof.Sedokeya amefafanua kuwa hakuna sharia inayozuia wabunifu na kinachotakiwa ni mtu kwenda serikalini katika mamlaka husika kwa ajili ya ushauri Zaidi anapofanya ubunifu kabla ya bidhaa yake kupeleka sokoni.
Mkurugenzi wa Sayansi ,Teknolojia na Ubunifu kutoka Wizara ya Elimu,Sayansi na Teknolojia Prof.Maulilio Kipanyula amesema mshindi wa kwanza mwaka huu atapatiwa zawadi ya Tsh.Milioni 5,mshindi wa pili milioni 3 na mshindi wa tatu milioni 2 huku washiriki wote kuendelezwa ambapo ni mikoa 16 na washiriki 862 walituma maombi ya ushiriki huku 70 wakipitishwa katika mashindano hayo.
Akizungumza kwa niaba ya Waandishi wa Habari,Sakina Abdulmasoud kutoka Uhuru Media amesema atahakikisha wanashirikiana na Wizara katika kutangaza ubunifu hapa nchini
Hadi sasa takriban wabunifu 200 wameshatambuliwa na serikali kupitia MAKISATU na kuingizwa kwenye kanzi data ikiwemo ubunifu wa MagnaTech ambaye sasa ni mbunifu mbobezi duniani katika usalama wa mitandao ambapo hivi karibuni amefungua ofisi nchini Dubai ikiwa na vijana wa Kitanzania saba huku mashindano ya MAKISATU mwaka huu yakitarajia kuanza Mei,15-20/2022 na yatakuwa ya nne tangu yaanze mwaka 2019
Post A Comment: