Na Benny Mwaipaja, Dodoma
WAZIRI wa Fedha na Mipango Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba (Mb), amekutana na kufanya mazungumzo na Chama cha Watoa Huduma wa Simu Tanzania (TAMNOA), na kuwaeleza kuwa kodi ya miamala ya simu na bando za mitandao inayotakiwa kuanza kutozwa na mitandao ya simu ni ya kizalendo inayolenga kila Mtanzania kuchangia mapato ya Serikali kwa ajili ya maendeleo ya nchi.

Dkt. Nchemba alisema kuwa Serikali imepanga kutekeleza miradi mingi ya maendeleo ya wananchi na inayohitaji fedha nyingi na kwamba jukumu la kukamilisha miradi hiyo ni la Watanzania wote wenye uchungu wa maendeleo.

“Fedha zitakazo patikana kwenye tozo hizo hazitatumika kulipa mishahara wala kugharamia matumizi mengine yoyote ya Serikali bali zitapelekwa moja kwa moja kutatua changamoto za afya, elimu, maji, miundombinu ya barabara, elimu na mingine mingi ikiwemo miradi ya kimkakati kama ujenzi wa reli ya kisasa na Bwawa la kuzalisha umeme la Julius Nyerere” alisema Dkt. Nchemba.

Dkt. Nchemba alisema kuwa jambo la kutia moyo ni kwamba Watanzania wengi wameunga mkono kutozwa kodi hiyo kwa kutambua umuhimu wa maendeleo yao ambayo kukamilika kwake kunahitaji mchango wao mkubwa.

“Kampuni za simu msichukulie makato haya kama kodi nyingine mnazowatoza wateja wenu bali Serikali iliamua kuweka makato haya kwenye miamala ya kuweka muda wa maongezi na kufanya miamala kwa njia ya simu ili kuwafanya Watanzania na watumiaji wengine wa simu kuchangia maendeleo ya nchi”alisisitiza Dkt. Nchemba.

Dkt. Nchemba alitoa muda wa siku 14 kuanzia tarehe 1 hadi 15 Julai, 2021, kwa watoa huduma wote wa Mitandao ya Simu kurekebisha mifumo yao na kuanza kutoza rasmi makato hayo ili Serikali ianze kukusanya fedha hizo ambazo amesema zitatumika kwa malengo yaliyokusudiwa ya kuwakwamua wananchi kutoka katika adha mbalimbali.

Kwa upande wao Chama cha Watoa huduma za mitandao ya simu, waliiomba Serikali kupitia Wizara ya Fedha na Mipango iwape muda wa kurekebisha mifumo yao itakayotumika kukusanya tozo hizo kwa kuwa zoezi hilo linahitaji muda wa kiufundi.

Akizungumza kwa niaba ya Chama hicho, Mkurugenzi wa Uhusiano wa Kampuni ya Simu ya Vodacom Bi. Roselynn Mworia, alisema kuwa chama chao kimeupokea mpango huo kwa mikono miwili na kuwataka wateja wao kuiunga mkono Serikali kwa kuendelea kutumia huduma za kupiga simu na kufanya miamala ya simu.

“Lengo la Serikali la kuamua kukusanya fedha za maendeleo kwa njia hiyo ni zuri kwani litaharakisha utekelezaji wa miradi ya huduma za kijamii, kwa kweli ni kodi ya kizalendo” alisema Bi. Mworia.

Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, hivi karibuni, lilipitisha tozo ya kuanzia shilingi 10 hadi shilingi 10,000 kutozwa katika kila muamala wa kutuma au kupokea pesa na kiwango cha shilingi 10 hadi 200 kwa siku kila mteja anapoongeza salio la muda wa maongezi kwenye simu ambapo kwa pamoja, Serikali inatarajia kukusanya wastani wa shilingi trilioni1.7 kwa mwaka.
Share To:

Post A Comment: