MSICHANA Rawan Dakik, (20) aliyepanda mlima Everest ambao ni mrefu kuliko yote duniani,  leo akipokelewa 


 na Naibu Waziri, Wizara ya Maliasili na Utalii, Mary Masanja kwenye uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Kilimanjaro, (KIA).




Aidha viongozi wengine waliokuwa uwanjani hapo ni Mkuu wa Mkoa wa Arusha, John Mongela, Mkuu wa wilaya ya Arumeru, Jerry Muro , Mbunge wa Arusha Mjini, Mrisho Gambo.



Mwenyekiti wa bodi ya udhamini ya Hifadhi za Taifa nchini, (TANAPA), Mkuu wa Majeshi wa Kwanza, Meja Jenerali, Mrisho Sarakikya na Kaimu Mkurugenzi wa Bodi ya Utalii nchini, (TTB), Beatrice James.




Dakik amewasilia uwanjani hapo leo majira ya saa 12.45 asubuhi akitumia ndege ya shirika la ndege ya Quater na kupata mapokezi hayo makubwa ambapo mbali na viongozi mbalimbali lakini pia alikuwa Mtanzania wa kwanza kupanda mlima Everest, mwaka 2012, Wilfred Moshi.




RAWAN ATEULIWA BALOZI WA UTALII



Naibu Waziri Masanja amemteua Rawan kuwa balozi wa utalii ambapo ameahidi kumwalika rasmi bungeni ili apewe nafasi aweze kutambuliwa sanjari na kwenye taasisi za utalii ili aweze kupata maelezo zaidi juu ya vivutio vivyopo nchini



Pia amekabidhi zawadi ya picha maalum inayoonyesha wanyama na mandhari nzuri ya moja ya hifadhi za hapa nchini.




"Kupitia tukio hili leo ninamtangsza rasmi, Rawan Dakik ni balozi wa hiari wa Utalii, Mtanzania wa kwanza mwanamke kupanda mlima Everest ambao ni mlima mrefu kuliko yote Duniani,"amesema Naibu Waziri Masanja na kuongeza.



"Sisi kama Watanzania tunamshukuru Mungu tumempokea mtoto wetu akiwa mwenye nguvu na afya. Niwapongeze wazazi wa  Rawan kwa kumsaidia binti yao kuweza kufikia malengo yake kwani tumeambiwa ameanza kupanda milima akiwa na miaka 12,", alisema Naibu Waziri Masanja.



  "Kwa kipindi cha miaka saba Rawan amekuwa akipanda milima mbalimbali barani Afrika ukiwemo mlima Kilimanjaro. Lakini leo nimpongeze kwa kuweza kufika kwenye kilele cha mlima mrefu duniani, Everest," amsema Naibu Waziri Madanja na kuongeza. 



"Nampongeza sana binti yetu, ametuheshimisha kama Taifa. Ameipa heshima Tanzania kwa kuitangaza kimataifa. Tumemuona mara zote alikuwa anapeperusha bendera ya Tanzania hivyo hata wale ambao walikuwa hawaijui Tanzania watakuwa wameijua kupitia Rawan,".



"Kupitia Rawan nawahamasisha Watanzania kupanda milima Kilimanjaro, vijana wa kike na wa kiume mjitokeze kupanda milima mbalimbali ndani na nje ya nchi ili rekodi aliyoivunja Rawsn wawepo Watanzania wazalendo wengine wa kuifikia,".



RAWAN ATAKA VIPAJI VYA VIJANA VITAMBULIWE 



Kwa upande wake, Rawan ametaka vipaji vya vijana nchini vitambuliwe , vithaminiwe, viheshimiwe, vitangazwe na viendelezwe kwani mafanikio ya vipaji hivyo yataleta heshima kwa Taifa.



"Nimepitia changamoto na hatari nyingi katika safari yangu ya kupanda mlima Everest, lakini kilichonipa nguvu ni kuona kuwa niliahidi kubeba wajibu wa kulipa Taifa langu la Tanzania heshima. Kwa kufika kwenye kilele cha mlima Everest nikiwa msichana wa kwanza mdogo kwa umri kutoka barani Afrika,". amesema  Rawan. 



Amesema anamshukuru Mungu kwa kumuwezesha kuweka historia hiyo huku akiwashukuru Watanzania kwa maombi na salamu za heri alizodai zilimtia moyo na kumfanya ajiamini zaidi na kuendelea kupanda mlima huo na kufanikiwa kufikisha bendera ya Tanzania kileleni.



 "Ushindi huu wa msichana wa kwanza mdogo wa miaka 20, kutoka Afrika Tanzania, kupanda mlima Everest ni faharu kubwa . Ninautoa kama zawadi kwa Watanxania wote na kwa mheshimiwa Rais wetu, mama yetu, Samia Suluhu Hassan,", amesema Rawan.



Amesema kuwa uzoefu wa kupanda mlima Everest aliupata kwa upanda mlima Kilimanjaro kwenye malango matatu tofauti ikiwemo like la Marangu, Machame na ya mzunguko wa kilele cha Kibo kwa upande wa Kaskazini.



"Mlima Kilimanjaro umenipa ujuzi mkubwa, Ujasiri mkubwa, utimamu wa mwili na akili ulionifanya niweze kufika katika kilele cha mlima Everest," amesema Rawan.



Aidha aliushukuru ujumbe wa serikali ulioongozwa na Naibu waziri, Masanja kwa mapokezi waliyompatia, Kamishina wa Uhusiano wa TANAPA, Paschal Shelutete pamoja na wote waliofika kumpokea vikiwemo vikundi vya ngoma za asili.




BABA YAKE ASEMA ATAMALIZIA MLIMA WA SABA MWAKANI



Kwa upande wake baba yake Rawan, Karim Dakik amesema kuwa Rawan ameshapanda vilele vya milima sita kata ya saba aliyopanga kupanda ambapo anatarajia kupanda  mlima Denali uliopo Alaska barani Amerika ya Kaskazini.



Alisema kuwa anatarajia kupanda mlima huo mwezi juni  mwakani wakati wa likizo ya masomo jambo litakalomwezesha kutimiza ndoto hiyo bila kuvuruga ratiba yake ya masomo.



"Furaha yetu kubwa zaidi ilijuwa Mei 23, mwaka huu. Saa 9:35 alfajiri kwa saa za Afrika Mashariki. Rawan alipofika kilele cha mlima Everest akiwa salama na kuiweka bendera ya Tanzania ambayo ilipepea kuisalimia Tanzania," amesema Dakik na kuongeza.



"Tupo na bendera hiyo iliyopepeakwenye mlima huo mrefu zaidi duniani ikituma salamu kwa nchi yetu ya Tanzania na wananchi wake kutokea juu ya kilele hicho ikisema kazi iendelee,".



"Amesema kuwa kama familia wanafurahi kuona binti yao anatumika kuitangaza Tanzania duniani hasa kwenye masuala ya utalii, upendo na amani sanjari na kutangaza utalii wa ndani, michezo ya upandaji milima ya ndani na nje ya nchi,".




MONGELA TUTAMTUMIA RAWAN KUHAMASISHA VIJANA



Mkuu wa mkoa wa Arusha, Mongela amempongeza Rawan kwa kuwa msichana wa kwanza kutoka Afrika kuweza kufika kwenye kilele cha mlima huo mrefu kuliko yote duniani.



"Tutamtumia Rawan kuhamasisha vijana wengine awajaze ujasiri waweze kupanda milima wakianza na ya kwetu Meru na Kilimanjaro," alisema Mongela.



Alisema hata yeye amehamasika ambapo mwaka huu atawaalika viongozi na marafiki zake wapande mlima Kilimanjaro.



TANAPA WAJIVUNIA MAFANIKIO YA RAWAN



Kwa upande wake Meneja Uhusiano wa TANAPA, Kamishina Msaidizi Mwandamizi wa Uhifadhi, Paschal Shelutete amesema kuwa wanajivunia kuwa sehemu ya mafanikio ya Rawan ambaye anaamini kufika kwake kwenye kilele cha Everest kumeutangaza zaidi mlima Kilimanjaro kimataifa.



"Rawan amefanya mazoezi kwenye mlima Kilimanjaro, na nyakati zote alipokuwa akihojiwa amekuwa akieleza hivyo jambo ambalo linatupa matumaini makubwa kuwa ujumbe huo umewafikia watu wengi wa mataifa mbalimbali hivyo wale wenye nia ya kupanda mlima Everest watakuja kufanya mazoezi kwenye Mlima Kilimanjaro ambao ni mlima mrefu kuliko yote barani Afrika," amesema Shelutete.



TTB: RAWAN KAUTANGAZA MLIMA KILIMANJATO VIZURI


 


Kaimu Mkurugenzi wa TTB, Beatrice alisema kuwa Taifa linajibunia kuwa na shujaa Rawan ambaye ni msichana mdogo ambaye kwa kupanda mlima Everest ameutangaza mlima Kilimanjaro kwa kiwango kikubwa.



"Mlikuwa mnaona taarifa zake kila zilipokuwa zikionyeshwa alikuwa na bebdera ya Taifa, lalini kikubwa kila alipokuwa akiongea alieleza alifanya mazoezi kwa kupanda mlima Kilimanjaro mara tano hivyo hiyo itawavuta watu wengi wanaotaka kupanda mlima Everest kuja Tanzania kufanya mazoezi kwenye mlima Kilimanjaro," alisema Beatrice.

Share To:

Post A Comment: