Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mashimba Ndaki akiongea na wananchi wa Kijiji cha Mpeta ambapo alieleleza kuwa zaidi ya Ekari Elfu Kumi na Nne (14000) zitegwe kutoka katika Ranchi ya Uvinza na zigawiwe kwa wananchi wanaoishi katika eneo la Mwandulubhantu na Kazaroho ili wazitumie kwa makazi na shughuli nyingine za kimaendeleo. Waziri Ndaki alitembelea Wilaya ya Uvinza iliyopo Mkoani Kigoma jana na kufanya maamuzi hayo kwa lengo la kumaliza mgogoro wa ardhi wa muda mrefu kati ya wananchi hao na Kampuni ya Ranchi za Taifa (NARCO).


Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mashimba Ndaki (kushoto) akiagana na mmoja kati ya Wazee wanaoishi katika Kijiji cha Mpeta aliyejitokeza kuhudhuria mkutano wa Waziri huyo na Wananchi wa Kijiji hicho uliofanyika Wilayani Uvinza Mkoani Kigoma jana. Katika Mkutano huo, Waziri Ndaki aliamua Ekari zaidi ya Elfu Nane (8000) zimegwe kutoka katika Ranchi ya Uvinza ili wakabidhiwe wananchi wanaoishi katika eneo la Mwandulubhantu lililopo katika kijiji cha Mpeta ili wazitumie kwa makazi na shughuli nyingine za maendeleo.

Wananchi wa Kijiji cha Mpeta wakiagana kwa furaha na Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mashimba Ndaki (katikati kulia) muda mfupi baada ya kumalizika kwa mkutano wa Waziri huyo na Wananchi wa Kijiji cha Mpeta uliofanyika Wilayani Uvinza Mkoani Kigoma jana.


 

Na Mbaraka Kambona, Kigoma

 

Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mashimba Ndaki ameielekeza Kampuni ya Ranchi za Taifa (NARCO) kutenga Ekari Elfu Kumi na Tano (15000) na wazigawe kwa Wananchi wa Vijiji viwili vya Mpeta na Chakulu vilivyopo Wilayani Uvinza, Mkoani Kigoma ili kutatua mgogoro wa ardhi wa muda mrefu baina ya wananchi hao na Kampuni hiyo. 

Ndaki alitoa maelekezo hayo jana katika ziara yake Wilayani Uvinza, Mkoani Kigoma kwa lengo kutatua mgogoro huo ardhi kufuatia wananchi wa vijiji hivyo kuvamia maeneo ya Ranchi ya Uvinza na kuishi humo kinyume na taratibu. 

Akiongea na wananchi wa vijiji hivyo kwa nyakati tofauti, Waziri Ndaki alisema kuwa Serikali imeamua kufikia maamuzi hayo ili wananchi hao waweze kujikita katika shughuli za maendeleo na kuachana na migogoro ya kila siku ambayo haina tija yoyote. 

“Hatupendi tuendelee na migogoro kwenye maeneo yetu, tunataka tumalize migogoro ili tuanze kufanya shughuli za maendeleo, kila mwananchi afanye shughuli yake bila bughudha yoyote,” alisema Ndaki. 

Aliongeza kuwa baada ya ugawaji wa maeneo hayo kukamilika Mkuu wa Wilaya ya Uvinza na timu yake watakwenda kufanya tathmini katika maeneo hayo na kuyafanyia mchakato wa kuyarasimisha ili kuwa Kijiji au Kitongoji. 

Alisisitiza kuwa pamoja na wananchi hao kuvunja Sheria, Serikali imeangalia maslahi mapana na ndio maana imeamua kutoa sehemu ya eneo katika ranchi hiyo ili wananchi hao waweze kuishi kwa utulivu na kuendelea na shughuli zao huku akiwaonya kuwa wasijaribu tena kuingia katika ranchi hiyo baada ya kugawa ekari hizo na atakayefanya hivyo anatafuta kesi. 

“Ranchi ni eneo la kufugia mifugo na sio eneo la kuishi watu au kulima humo, atakayejaribu kuingia tena ananitafuta kesi, tumewapa maeneo hayo ili mkae humo, atakayetaka kufuga aje sisi tutampa eneo la kukodisha kwa bei ya Serikali ili aweze kufuga kisasa, kulima malisho na kuongeza tija ya mifugo yake,” alisisitiza Ndaki. 

Mkuu wa Wilaya ya Uvinza, Mwanamvua Mrindoko baada ya kumshukuru Waziri Ndaki kwa uamuzi huo naye aliwasisitiza wananchi hao kutoendelea kuvamia maeneo ya ranchi hiyo ili kuepukana na migogoro isiyo na tija na badala yake watumie maeneo hayo waliyopewa kujiletea maendeleo yao. 

Naye, Mwenyekiti wa Kijiji cha Chakulu, Mohamed Baswage aliishukuru Serikali kwa tamko hilo la kuwapa eneo wananchi wa Kijiji hicho huku akisema kuwa uamuzi huo utawasaidia wao kusukuma maendeleo yao kwa pamoja wakishirikiana na Serikali.

Share To:

Post A Comment: