Mwenyekiti wa UVCCM Mkoa wa Singida Dkt. Denis Nyiraha 

 
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,  Dkt. John Pombe Magufuli  akimuapisha Dkt. Bashiru Ally Kakurwa kuwa Balozi na Katibu Mkuu Kiongozi.


Na Dotto Mwaibale, Singida

UMOJA wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM) Mkoa wa Singida umempongeza Dkt. Bashiru Ally Kakurwa kwa kuteuliwa na Rais John Magufuli kuwa Balozi na Katibu Mkuu Kiongozi.

Akizungumza na waandishi wa habari jana Mwenyekiti wa UVCCM Mkoa wa Singida Dkt. Denis Nyiraha alisema uteuzi  huo  wa Bashiru ni sahihi kutokana na kazi nzuri alizozifanya  ndani ya chama kwa nafasi ya Katibu Mkuu.

Nyiraha alisema Bashiru akiwa Katibu Mkuu wa CCM alifanikiwa kurejesha mali za chama zilizokuwa mikononi mwa watu wengine kinyume na utaratibu.

" Pamoja na kuzirejesha  mali  hizo Bashiru alifanikisha chama hicho kupata ushindi katika uchaguzi wa Serikali za mtaa uliofanyika mwaka juzi ." alisema Nyiraha.

Aidha Nyiraha alisema katika kukiongoza chama hicho kwa  nafasi hiyo ya Katibu Mkuu  CCM ilipata  ushindi mkubwa kwenye uchaguzi mkuu 2020.

Nyiraha alitaja mafanikio mengine ya Dkt.Bashiru kuwa ni kusimamia nidhamu ya utumishi ndani ya chama na nje ya chama.

" Hakika tunayo imani  Dkt. Bashiru ataisimamia Serikali ipasavyo kutimiza majukumu yake kama alivyofanya akiwa katika nafasi hiyo kubwa ndani ya chama." alisema Nyiraha.

Share To:

Post A Comment: