Naibu Kamishna wa Uhifadhi wa Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro Dkt. Christopher Timbuka (katikati) akiongozana na Kamishna Msaidizi Mwandamizi (Maendeleo ya Jami) Mdalla Fedes (kushoto) na watumishi wengine kukagua shamba lililopandwa  Mazao katika Kijiji cha Mang’ola juu Wilayani Karatu mkoani Arusha.
Naibu Kamishna wa Uhifadhi wa NCAA Dkt. Christopher Timbuka (Kulia) akisikiliza maelezo kuhusu mradi wa shamba la Mang’ola kutoka kwa Kamishna Msaidizi Mwandamizi (Maendeleo ya Jamii) Bw. Mdalla Fedes.
Mwenyekiti wa Kijiji cha Sendui Wilayani Ngorongoro Bw. Meeli Saruni  akimuelezea Naibu Kamishna Dkt Timbuka jinsi wananchi wake walivyopokea mradi wa kilimo katika shamba lililoko Mang’ola juu Wilayani Karatu.
Naibu Kamishna wa NCAA Dkt. Christopher Timbuka (Kulia) akitoa maelekezo kwa watumishi wa Idara ya Maendeleo ya jamii kuhakikisha kuwa wanashirikiana na wananchi wanaolima eneo hilo hasa katika udhibiti wa Wanyamapori wanaongia kwenye mashamba ya wananchi wanaolima nje ya Hifadhi.
Sehemu ya Shamba ambalo wananchi kutoka Kijiji cha Sendui Wilayani Ngorongoro wamelima na kupanda mazao ya Mahindi na Maharage.

Naibu Kamishna wa Mamlaka ya Hifadhi Ngorongoro anayesimamia (Uhifadhi, Utalii na Maendeleo ya Jamii) Dkt. Christopher Timbuka amewapongeza wananchi waliohamasika na mradi wa shamba la Mang’ola juu Wilayani Karatu lililoanzishwa kwa lengo la kuwasaidia wananchi wanaoishi ndani ya Hifadhi ya Ngorongoro.


Dkt Timbuka amesema hayo leo tarehe 19 februari, 2021  wakati akikagua shamba hilo lenye ukubwa wa ekari 53 ambalo NCAA ilisaidia upatikanaji wake  kwa lengo la kuwasaidia wananchi waishio ndani ya Hifadhi ya Ngorongoro kukodi na kulima mazao mbalimbali ikiwemo mahindi na Maharage kwa ajili ya kuwawezesha kupata Chakula.

“Kwa kuwa Sheria hairuhusu kulima ndani ya Hifadhi, Serikali kupitia Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro ilitafuta eneo hili nje ya Hifadhi ili Wananchi waweze kukodi na kulima mazao mbalimbali yatakayowawezesha kupata chakula na kuepuka kutegemea mifugo pekee, mradi huu ndio umeanza msimu huu na kadri unavyoendelea tunaamini wananchi wengi watahamasika kulima kwa kuwa eneo lipo la kutosha” alisema Dkt Timbuka.

Kwa upande wake Kamishna Msaidizi mwandamizi anayesimamia Idara ya Maendeleo ya Jamii Bw. Mdala Fedes ameeleza kuwa, mradi huo ulianza kwa kutoa elimu na hamasa kwa Wananchi wa vijiji 25 vilivyopo ndani ya Hifadhi juu ya uwepo wa fursa hiyo ambapo wananchi 246 kutoka vijiji mbalimbali ikiwemo Sendui, Bulati, Misigyo na Olpiro walikubali kuanza kulima na tayari kati ya ekari 53 zilizolimwa msimu huu, ekari 47 tayari zimeshapandwa mazao mbalimbali.

“Lengo letu ni kutoa hamasa zaidi kwa wananchi na tumewaunganisha na wataalam wa kilimo ili waelimishwe kulima kitaalam na kupata mazao ya kutosha kuliko kutegemea Serikali moja kwa moja, lengo letu ni kuhakikisha kuwa mwakani hali ya hewa ikiruhusu wananchi walime ekari 500 kwa kuwa eneo lipo la kutosha” aliongeza Mdalla.

Mwenyekiti wa Kijiji cha Sendui kata ya Alaelelai Wilaya ya Ngorongoro Bw. Meeli Saruni ameishukuru Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro kwa kuwasaidia kupata eneo hilo na kuahidi  kuhamasisha wananchi wa vijiji vingine waweze   kujitokeza kwa wingi.

Share To:

Post A Comment: