Picha ya jengo la utawala la kituo kipya cha Mabasi Katumba Azimio Manispaa ya Sumbawanga pindi litakapokamilika ujenzi wake mwezi Disemba 2019.
 Mkuu wa mkoa wa Rukwa Mh. Joachim Wangabo (katikati) akikata utepe kuashiria uzinduzi wa ujenzi wa kituo kipya cha mabasi cha Katumba Azimio katika Manispaa ya Sumbawanga.
Mkuu wa mkoa wa Rukwa Mh. Joachim Wangabo (kulia) akimpongeza mkurugenzi wa manispaa ya Sumbawanga James Mtalitinya (kulia) wakati wa hafla fupi ya uzinduzi wa ujenzi wa kituo kipya cha Mabasi Katumba Azimio Manipsaa ya Sumbawanga.
Mkuu wa mkoa wa Rukwa Mh. Joachim Wangabo amepongeza juhudi zinazofanwa na Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Sumbawanga katika kukusanya mapato pamoja na kuwa mbunifu wa kuongeza vyanzo mbalimbali vya mapato ili kuweza kutatua na kukamilisha miradi mbali mbali ya manispaa hiyo.
Amesema kuwa kukamilika kwa stendi hiyo ya kisasa kutaongeza ukusanyaji wa mapato wa karibu asilimia 46 ya mapato ya sasa ambapo manispaa hiyo ilikisia kwa mwaka wa fedha wa 2018/2019 ikusanye shilingi 2,212,104,000 na hadi kufikia mwezi machi 2019 ilikuwa imekusanya shilingi 2,424,032,802.71 ambayo ni sawa na asilimia 110 ya makusanyo.
“Hii stendi ikimalizika mapato ya kutoka hapa itakuwa bilioni 1, sasa hii ni karibu asilimia 46 ya mapato yote ya manispaa kwa sasa hivi, hamuoni kwamba mapato ya manispaa yataongezeka kwa kasi kubwa sana na kwa hali hiyo hata waheshimiwa madiwani wataweza kutekeleza mipango yao vizuri na kwa ukamilifu sana na watakaonufaika ni sisi wananchi wote ndani ya Manispaa, “Alisema.
RC Wangabo ametoa kauli hiyo wakati wa hafla fupi ya uzinduzi wa ujenzi wa kituo kipya cha kisasa cha mabasi kitakachojengwa katika eneo la Katumba azimio lililopo kilomita 12 kutoka Sumbawanga mjini, ambapo mradi huo ukikamilika utaiingizia manispaa ya Sumbawanga Shilingi 1,027,800,000 kwa mwaka.
Aidha, Aliwataka wakurugenzi wa halmashauri nyingine za mkoa huo kuipa kipaumbele miradi ya kimkakati, miradi ambayo huleta fedha nyingi kwa wakati mmoja kwani kwa kufanya kutazifanya halmashauri hizo kuweza kutatua kero nyingi za wananchi pamoja na kuboresha huduma mbalimbali za kijamii kwa wananchi.
Kwa upande wake Mkurugenzi wa Manispaa ya Sumbawanga James Mtalitinya alisema kuwa miundombinu itakayojengwa katika eneo hilo ni pamoja na Eneo la kuegeshea mabasi ya ndani na nje ya mkoa, bajaji, bodaboda, taksi na baiskeli, vyumba vya maduka, jengo la utawala, kituo kidogo cha polisi, mama lishe, choo cha kulipia, uzio, Taa, mifereji, vyumba kwaajili ya benki na ATM’s na vyumba vya mazoezi (Gyms)
“Mzabuni aliyepatikana kwaajili ya ujenzi wa kituo cha Kisasa cha Mabasi Katumba azimio ni Sumry Enterprises Ltd. Eneo ambalo litatumika kwaajili ya Ujenzi wa Stendi ni ekari 10 na ekari 12 zitakuwa ni kwaajili ya mipango ya halmashauri ya hapo baadae. Mradi huu ni chanzo cha mapato ambacho kitaweza kutuingizia fedha itakayotumika kujenga au kumalizia miradi mbalimbali ya maendeleo iliyopo ndani ya Manispaa na Kuboresha huduma mbalimbali.” Alisema.   
Kwa mwaka wa fedha 2018/2019 Manispaa ya Sumbawanga iliweka bajeti ya ujenzi wa kituo cha kisasa cha mabasi Katumba Azimio kupitia fedha za Mradi wa Uimarishaji miji (ULGSP) na kumpata mkandarasi Sumry Enterprises Ltd ambaye atahusika na ujenzi huo utakaogharimu shilingi 5,955,363,986 bila ya VAT na kutegemewa kumalizika mwezi Disemba 2019.
Share To:

Post A Comment: