Maadhimisho ya Siku ya Uhuru wa Vyombo vya Habari Duniani 2019 yameanza hii leo jijini Dodoma ambapo yanafanyika kitaifa kwa awamu ya pili mwaka huu. Kilele cha maadhimisho hayo hufanyika kila mwaka Mei 03 ambapo wadau wa habari hukutana pamoja kujadili masuala mbalimbali yanayohusu uhuru wa vyombo vya habari/ wanahabari katika gurudumu la maendeleo.
Picha na KD Mula, Funguka Live Blog
Mkurugenzi wa MISA Tanzania, Sengiyumva Gasirigwa akiwasilisha mada kwa niaba ya makundi ya washiriki kwenye maadhimisho hayo. 
Lilian Kallaghe kutoka taasisi ya SIKIKA akiwasilisha mrejesho wa majadiliano kwa niaba ya washiriki wengine. 
Mwakilishi wa shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia masuala ya elimu (UNESCO) nchini Tanzania, Nancy Kaizirege akitoa salamu za shirika hilo kwenye ufunguzi wa maadhimisho hayo.
Washiriki wa maadhimisho hayo walisimama kwa muda kama ishara ya kumuombea aliyekuwa Mwenyekiti wa Wamiliki wa Vyombo vya Habari Tanzania (MOAT) na pia mmiliki wa makampuni ya IPP, Mzee Reginald Mengi aliyefariki usiku wa kuamkia leo akiwa nchini Dubai akiwa na miaka 75.
Mkurugenzi wa Taasisi ya Vyombo vya Habari Kusini mwa Afrika (MISA) tawi la Tanzania, Sengiyumva Gasirigwa (katikati) akimsikiliza kwa umakini Mweka Hazina wa taasisi hiyo, Michael Gwimile kwenye maadhimisho hayo (kulia).
Mwenyekiti wa Taasisi ya Vyombo vya Habari Kusini mwa Afrika (MISA) tawi la Tanzania, Salome Kitomari wakifuatilia mada kwenye maadhimisho hayo.
Baadhi ya washiriki wakifuatilia mada kwenye maadhimisho hayo.
 Wanahabari kutoka vyombo mbalimbali vya habari nchini Tanzania.
Baadhi ya washiriki wa maadhimisho hayo akiwemo Mkurugenzi wa kampuni ya Uhuru Media Group, Ernest Sungura wakifurahia jambo kwenye maadhimisho hayo.
Wahadhiri kutoka Chuo Kikuu cha Dar es salaam wakifuatilia kwa umakini uwasilishaji mada kwenye maadhimisho hayo.
Washiriki wa maadhimisho hayo akiwemo Joyce Shebe kutoka Clouds Media Group (kushhoto) wakifuatilia mada kwa umakini.
Na George Binagi-GB Pazzo, BMG

Maadhimisho ya Siku ya Uhuru wa Vyombo vya Habari Duniani 2019 yameanza hii leo jijini Dodoma, yakilenga kujadili masuala mbalimbali yanayohusu uhuru wa vyombo vya habari na wanahabari.

Msisitizo mkubwa umetolewa kwa wadau wa habari kujadili viashiria vya kushuka kwa uhuru vya habari nchini Tanzania na namna ya kuviepuka hususani baadhi ya waandishi wa habari kupotea, kukamatwa na kushikiliwa kwa muda na mamlaka nchini.

Aidha wanahabari pamoja na wahariri wamepewa changamoto ya kuhosi sababu za Tanzania kushuka kwa nafasi 25 kutoka nafasi ya 93 mwaka jana hadi nafasi ya 118 mwaka huu kwenye orodha ya uhuru wa vyombo vya habari duniani.

“Tunapaswa kuhoji kwa nini tumeshuka kwenye nafasi ya uhuru wa vyombo vya habari duniani, mwaka jana tulishuka kwa nafasi 10 kutoka nafasi ya 73 hadi nafasi ya 93 na mwaka huu tumeshuka kutoka nafasi ya 93 hadi nafasi ya 118”, wamehoji washiriki kwenye maadhimisho hayo.

Mkurugenzi wa MISA Tanzania, Sengiyumva Gasirigwa amesisitiza waandishi wa Habari Tanzania kuongeza kiwango chao cha elimu ili kuendana na matakwa ya sheria hatua itakayosaidia kufanya shughuli zao kwa mujibu wa taaluma bila vikwazo kutoka kwa mamlaka za kisheria.

Mwakilishi wa shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia masuala ya elimu (UNESCO) nchini Tanzania, Nancy Kaizirege amesema waandishi wa habari wanapaswa kushikamana pamoja ili kulinda usalama wao.

“Waandishi 99 waliuawa mwaka jana wakiwa kazini na tangu mwaka 1994 hadi 2018 jumla ya waandishi 1,377 wameuawa kutokana na majukumu hayo”, amebainisha Kaizirege akieleza jinsi usalama wa waandishi wa habari ulivyo mashakani.

Taasisi mbalimbali zimeshiriki kwenye maandalizi ya maadhimisho hayo ikiwemo MISA Tanzania, Internews, IMS, UTPC, TMF, TEF, UK Aid, TAMWA, MCT, UN Tanzania, FES, Unesco na Serikali ya Tanzania, kauli mbiu ikiwa ni “Vyombo vya Habari kwa Demokrasia, Tasnia ya Habari na Uchaguzi nyakati za upotoshwaji wa taarifa” ambapo kilele cha maadhimisho hayo hufanyika kila mwaka Mei 03.
Share To:

Post A Comment: