Waziri wa Maliasili na Utalii, Dkt.Damas Ndumbaro  na Katibu Mkuu, Wizara ya Maliasili na Utalii, Dkt. Allan Kijazi na Kamishna wa uhifadhi Wakala wa huduma za misitu Tanzania TFS Prof. Dos Santos Silayo wakimsikiliza  Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Mary Francis Masanja,wakati akieleza  kwa viongozi hao kwenye maonesho ya utalii EAC.

Kamishna wa uhifadhi Wakala wa huduma za misitu Tanzania TFS Prof. Dos Santos Silayo akibadilishana mawazo na mmoja kati ya wadau wa sekta ya misitu Tanzania.

 

 

Jane Edward-Arusha

Katika kuunga mkono jitihada za Rais wa Tanzania Samia Suhulu Hassan katika kutangaza utalii ndani na nje ya nchi,Wakala wa huduma za misitu Tanzania (TFS) imeanza kutoa ofa kwa wananchi wa jumuiya ya Afrika mashariki kutembelea maeneo ya ikolojia na kujionea fursa zilizopo.

Kauli hiyo inatokana na kuwepo kwa maonyesho ya kwanza ya utalii yaliyoandaliwa na Jumuiya ya Afrika mashariki kwa kushirikiana na jamhuri ya muungano wa Tanzania, yaliyofanyika Makao makuu ya jumuiya hiyo Mkoani Arusha. 

Akizungumza na waandishi wa Habari Kamishna wa uhifadhi Profesa Dos Santos Silayo amesema serikali imekuwa ikifanya jitihada mbalimbali katika kuhakikisha maeneo ya ikolojia, misitu yanatembelewa ili kuweza kuionyesha dunia vivutio vilivyopo sambamba na kuunga mkono juhudi za Mheshimiwa Rais katika kutangaza utalii katika nyanja zote.

"Tumeshiriki katika Maonyesho haya ya Afrika mashariki ili kuionyesha Afrika mashariki na dunia mambo tuliyoko nayo sisi kama wakala wa huduma za misitu Tanzania"Alisema Prof Silayo

Ameongeza kuwa nchi zetu za Afrika mashariki zinaegemea sana utalii wa wanyama pori lakini kwenye utalii wa ikolojia haujapewa nafasi kubwa na TFS inataka wananchi watembelee na waone bainoyuwai zilizopo na hata kugusa maeneo hayo.

Profesa Silayo ameyataja baadhi ya maeneo yatakayo tembelewa katika ofa hizo ni pamoja na Bagamoyo ngome kongwe, Kaole lakini pia misitu ya mikoko, misitu ya pugu, panzi wenye bendera ya Taifa na kuwataka watanzania pia kutumia fursa hiyo.

Amewataka pia wananchi wa Arusha kujitokeza kutumia fursa hiyo ambapo wataenda ziwa duluti na kutembelea misitu ya mlima Meru ambapo ofa hizo zitaisha tarehe 16 na kama kuna ambao hawakuweza kufanya utalii huo kutokana na sababu mbalimbali basi wawasiliane na TFS ili kupata utaratibu mwingine.

 

Share To:

Teddy Kilanga

Post A Comment: