Jaji Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mhe. Joaquine De Mello akifungua mkutano wa mkutano kwa wadau wanaohusika na utoaji haki jinai kwa watoto wanaopitia ukatili wa kingono na amesisitiza kumlinda mtoto dhidi ya ukatili wa vitendo vya kikatili wa kingono.
Mkurugenzi Mtendaji wa shirika lisilo la kiserikali la Jukwaa la Utu wa Mtoto (CDF) Bwn. Koshuma Mtengeti akitoa maelezo kwa washiriki wa mkutano jinsi shirika lake linavyofanya kazi katika kulinda utu wa mtoto wa kitanzania.
Mmoja wa Wawezeshaji wa mkutano huo Mhe. Mwanabaraka Mnyukwa, Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Mwanza akitoa salamu za Mkuu wa Chuo cha Uongozi Mahakama Lushoto wa wadau.

Picha mbalimbali za washiriki wa mkutano huo kutoka katika taasisi mbalimbali za utoaji haki nchini wakifuatilia mijadala iliyokuwa inaendelea.


 Rosena Suka, Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto

JAJI wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Joaquine De Mello, leo Oktoba 20, 2021 amefungua mkutano kwa wadau wanaohusika na utoaji haki jinai kwa watoto wanaopitia ukatili wa kingono uliofanyika katika hoteli ya St. Gaspar jijini Dodoma. Mkutano huo umeandaliwa na Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA) kwa kushirikiana na Shirika lisilo la Kiserikali la Jukwaa la Utu wa Mtoto (CDF) la nchini Tanzania na Taasisi ya Irish Rule of Law International (IRLI) chini ya ufadhili wa Ubalozi wa Ireland nchini Tanzania.

Akizungumza kwa niaba ya Waziri wa Katiba na Sheria katika ufunguzi wa mkutano huo wa siku mbili ambao umehudhuriwa na majaji, mahakimu,maafisa wa afya, Maafisa ustawi wa jamii, waendesha mashataka na polisi Mhe. De Mello alieleza kwamba lengo kuu la mkutano huo ni kujadili kwa uwazi na kwa kina mizizi au vyanzo vya tatizo hili na kuweka nia na mikakati thabiti ya pamoja ya kuzuia vyanzo na viashiria vya tatizo hilo.

Mhe. De Mello aliendelea kwa kusema kwa hivi karibuni unyanyasaji wa kingono unaendelea kuchukua sura mpya ukizingatia kwa ukuwaji wa utandawazi na matumizi makubwa ya mitandao inayopelekea mtoto kila siku kuwa hatarini kunyanyasika kingono kutokana na mabadiliko ya kitechnologia pamoja na tabia za binadamu.

Katika mkutano huo pia Mhe. De Mello alitoa rai kwa vyombo vya utoaji haki kuwa ushahidi wa kesi hizi lazima uthibitike na kufanyiwa utafiti na uchunguzi wa kina pamoja na mashahidi ambao wanatakiwa kuwa tayari kuithibitishia mahakama, na aliendelea kuviasa vyombo hivyo kuacha kuchelewesha kutoa haki pale upelelezi wa matukio ya unyanyasaji wa kijinsi dhidi ya watoto waathirika wa ukatili dhidi ya matendo ya kingono unapokuwa umekamilika.

"Upelelezi unaocheleweshwa ndio unaopelekea haki inayocheleweshwa"

Akiongea kwa niaba ya Mkuu wa Chuo, Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto, Mhe. Mwanabaraka Mnyukwa, Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Mwanza alieleza kwa washiriki hao kuwa Chuo kwa kushirikiana na wafadhili mbalimbali ndani ya Tanzania na nje kwa kujali haki za mtoto kimeweza kuendesha mafunzo kwa wadau mbalimbali wa sheria kwa Majaji, Mahakimu wa ngazi mbalimbali, Mawakili wa Serikali, Waendesha Mashtaka, Maafisa Ustawi wa Jamii na Mawakili wa kujitegemea. Alifafanua zaidi kwa kuwashukuru wafadhili mbalimbali waliofadhili mafunzo hayo ambao ni Shirika linaloshughulikia haki ya mtoto duniani (UNICEF) ambapo kilifadhili jumla ya wadau mia saba arobaini na tano, Chama cha Mawakili Taanganyika chini ya ufadhili wa Shirika la Pact Kizazi Kipya kupitia Shirika la Msaada wa watu wa Marekani (USAID) wadau mia mbili ishirini na mbili na majaji sitini na tano.

Sambamba na hayo Mhe. Mnyukwa aliendelea kwa kusema Chuo kimekuwa kikifanya tafiti kadhaa juu ya uendeshaji wa mafunzo na kupelekea kupatikana kwa kitabu chenye mkusanyiko ya mashauri ya mtoto. Kitabu hiki kinasaidia katika katika utoaji wa haki katika mashauri ya mtoto.

Mhe. Mnyukwa alimalizia hotuba kwa kuushuruku uongozi mzima wa CDF kwa kuona mchango na jitihada zinazofanywa na IJA kwenye masuala ya kulinda haki za mtoto na kuamua kufanya ushirikiano katika kuendesha mkutano huu pia amezikaribisha taasisi nyingine ambazo zinapenda kufanya kazi na IJA.

Naye Mkurugenzi Mtendaji wa taasisi ya CDF Koshuma Mtengeti alielezea kwa washiriki wa mkutano huo kuwa malengo makuu ya shirika hilo ni kutekeleza mipango ya programu mbalimbali za kukuza, kutetea na kuboresha ustawi wa mtoto wa kitanzania.

Bwana Koshuma aliendelea kwa kusema mkutano huu unafanyika baada ya mradi wa Majaribio kushughulikia Ukatili wa Kijinsia kupitia Kujenga Uwezo wa Taasisi kwa Mtanzania Mfumo wa Haki ya Jinai katika Wilaya ya Mpwapwa, ambao ulifadhiliwa na ubalozi wa Ireland nchini Tanzania kwa kupitia taasisi yake ya ya Irish Rule of Law International (IRLI)
Share To:

Post A Comment: