Kamati ya kudumu ya baraza la wakilishi ya kusimamia ofisi za viongozi wakuu wa Kitaifa imefanya ziara katika ofisi za NEMC jijini Dar es salaam ili kujifunza kuhusu uhifadhi na Usimamizi wa Mazingira kuona changamoto ambazo NEMC inakabiliana nazo katika kusimamia mazingira nchini pamoja na hatua zinazochukuliwa kukabiliana nazo.

Aidha Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa kwanza wa Rais Mhe. Dkt. Saada Mkuya Salum amesema lengo kuu la ziara ya kamati ni kuweza kubadilishana mawazo na kuona kwa jinsi gani kazi zitaweza kufanyika ingawa zinasimamiwa kwa utofauti wa pande mbili za Muungano lakini athari za kimazingira zinafanana. ‘’ Tumepata fursa ya kukaa pamoja na kuona ni kwa namna gani tunaweza kuendeleza kazi zetu, ikiwemo kujua changamoto ambazo NEMC inazikabili na kwa vipi wanaweza kuzitatua na sisi kwa upande wetu tumeweza kujifunza mambo mengi ikiwemo ni jinsi gani ya kutengeneza mbinu mbalimbali za kuweza kusimamia masuala ya mazingira Zanzibar.’’

Kwa upande wake Mkurugenzi mkuu wa Mamlaka ya usimamizi wa Mazingira Zanzibar, Bw. Shekhe Juma amesema kikao kimekuja na matarajio na hatua zinazofaa kuchukuliwa ikiwemo kuongeza ushirikiano na Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC)katika eneo la tafiti za Mazingira Zanzibar katika visiwa vidogovidogo, ambavyo zinaathiriwa sana na mmomonyoko. ‘’Athari za kimazingira hazina mipaka, Bahari tunayoitumia Zanzibar wavuvi wetu wanavua katika maeneo yaleyale ambayo pia waTanzania Bara wanavua, tumekubaliana kuona namna ambavyo tutakuwa na Sheria ambazo zinalingana ili kuongeza ufanisi katika usimamizi wa mazingira.’’

Naye Mkurugenzi Mkuu wa NEMC Dkt. Samuel Gwamaka amesema "tumetembelewa na wajumbe, wawakilishi ambao wanaunda kamati ya mazingira kwa upande wa baraza la Wakilishi Zanzibar, sisi kama Baraza la Mazingira, tumewaeleza mfumo wa baraza ulivyokaa, jinsi tunavyofanya kazi na suala zima la tafiti hasa kisiwa cha Zanzibar na Pemba". ‘’Kama Baraza tumejifunza mengi kutoka kwao na baadhi ya changamoto ambazo tumejadili ni pamoja na tafiti hasa katika kisiwa cha Zanzibar na Pemba. Kwasababu ya mabadiliko ya tabia Nchi tayari kuna visiwa vinaendelea kulika, miradi ya jinsi hiyo sio miradi ya kuiacha upande wa ZEMA lakini na sisi NEMC tunahusika kwasababu bahari haina mipaka, athari zozote zinazoweza kutoka Zanzibar zinatugusa na sisi moja kwa moja. Kwahiyo tumekubaliana kwamba sisi kama Baraza tutakuwa na tafiti za pamoja na ZEMA ikiwa ni pamoja na kuweza kusaidia kwa upande wa uwezo ili waweze kuandika miradi kutoka kwenye mashirika ya kimataifa" aliongezea Dkt. Gwamaka.

Share To:

Post A Comment: