Waziri  wa Habari, Utamaduni Sanaa na Michezo. Mhe, Innocent Bashungwa akizungumza

Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe. Innocent Bashungwa aliyevalia jezi ya timu ya Taifa ya Mpira wa Miguu (Taifa Stars) katikati  akiwa katika picha ya pamoja na viongozi mbalimbali wa mpira wa soka na wachezaji wa timu za taifa za wanawake (Twiga Stars na Tanzanite) alipowatembelea wakiwa mazoezini katika viwanja vya  Kidongo chekundu maarufu kama  JK Park jijini Dar es Salaam.


Na John Mapepele, WHUSM

 

Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo kwa kushirikiana na Wizara ya Afya leo Agosti 28, 2021 imeratibu zoezi la hiari la siku mbili kwa timu za Taifa za michezo na wadau wote wa michezo upatiwa chanjo ya Uviko-19 jijini Dar es Salaam ili kujikinga na ugonjwa huo.

 

Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo. Mhe, Innocent Bashungwa amesema makundi hayo yamependekezwa kupewa kipaumbele kwa kuzingatia, pamoja na mambo mengine, umuhimu wao kwa jamii na ukweli kwamba kwa mazingira ya kazi zao, wako katika hatari ya kuambukizwa.

 

“Ninapenda tena leo kuendelea kusisitiza na kuhamasisha wanahabari, wanautamaduni, wasanii na wanamichezo wenzangu kuendelea kupata huduma ya chanjo. Sekta zetu zinahudumia wananchi na hivyo kulazimika kukutana na makundi ya watu mara kwa mara. Kutokana na hivyo tuna hatari kubwa ya kuambukizwa, ama sisi wenyenyewe au kuambukiza wananchi ambao ndio wadau wetu wakubwa tunaowapa huduma. Kwa vyovyote vile ni lazima tujikinge lakini pia tuwakinge wadau wetu”. Amefafanua  Mhe. Bashungwa

 

Amesema ili kufanikisha zoezi hilo vimefunguliwa vituo maalum ndani ya uwanja wa Mkapa na Uhuru vitakavyokuwa vikitoa huduma ya chanjo hiyo kuanzia saa 3 asubuhi kwa siku zote mbili  ili kutoa fursa kwa wadau wote kupata huduma ya chanjo.

 

Ameushukuru Uongozi wa Klabu ya Simba kwa kuwapa chanjo wachezaji wao.

Aidha, amepongeza Klabu ya Yanga ya kutumia wiki yao ya wananchi kuhamasisha na kupata chanjo na kulifanya zoezi hilo la uchanjaji kuwa miongoni mwa shughuli zao muhimu watakazo zifanya siku hiyo ambapo pia ametoa wito kwa vilabu vingine vya soka nchini kuhamasika na kuwapatia chanjo wachezaji na watumishi wao.

Mkurugenzi wa Michezo nchini Yusuph Singo Omary amemhakikishia  Mhe. Waziri kuwa maandalizi yote ya zoezi la chanjo yamekamilika na tayari wadau mbalimbali wa michezo wamepongeza hatua ya Serikali kupitia Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo kuendelea kuwapa kipaombele wadau ili wajikinge.

Ametoa wito kwa Wasanii, Wanahabari na Wachezaji kwa hiari yao kujitokeza na kutumia fursa hii kipata chanjo ili kujikinga na kuwakinga wengine na ugonjwa wa UVIKO 19

 

 

 

 

Share To:

TANGA RAHA BLOG

Post A Comment: