Na John Walter-Babati

Mbunge wa Babati Vijijini Mh Daniel Sillo amewaambia Wananchi wa Jimbo lake kuwa serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania chini ya Rais wa wamu ya sita Samia Suluhu Hassan, imedhamiria kuboresha miundombinu ya barabara,afya,umeme na maji katika maeneo yao hivyo kwa sasa wasubiri utekelezaji.

Mheshimiwa Sillo akizungumza na wananchi katika kata za Ayasanda na Riroda, amesema Bunge katika bajeti kuu ya serikali iliyopitishwa na Bunge mwezi uliopita imeongeza tozo kwenye simu na mafuta ambapo pesa zitakazopatikana zinakwenda TARURA kwa ajili ya barabara.

Ameongeza kuwa Rais Samia suluhu Hassan ametoa shilingi milioni mia tano kwa wakala wa barabara nchi nzima ili kutengeneza barabara haswa za Vijijini.

Amewataka Wananchi jimboni humo kuendelea kuiunga mkono serikali kwa kufanya kazi kwa bidii na kuacha kulalamika.

Mheshimiwa Daniel Sillo anafanya ziara katika kata za jimbo hilo kutoa shukrani kwa Wananchi kwa kumuamini kuwatumikia na  ameshafanya ziara katika kata za Mwada,Nkaiti,Kisangaji,Magara, Riroda na Ayasanda.
Share To:

Post A Comment: