Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Chama Cha Mapinduzi CCM, imemteua Mkuu wa Wilaya ya Iramba Mkoani Singida, Kenani Kihongosi kuwa Katibu Mkuu wa Umoja wa Vijana wa Chama hicho UVCCM.

Kihongosi ameteuliwa kushika nafasi hiyo akichukua nafasi ya Raymond Mwangala ambaye ameteuliwa hivi karibuni na Rais Samia Suluhu Hassan kuwa Mkuu wa Wilaya ya Ngorongoro Mkoani Arusha.

Akizungumza na Wandishi wa Habari jijini Dodoma, Katibu wa NEC Itikadi na Uenezi, Shaka Hamdu Shaka amesema maamuzi hayo yamefanyika leo kufuatia kikao cha kawaida cha Kamati Kuu kilichoketi leo chini ya Mwenyekiti wake, Rais Samia Suluhu Hassan.

Shaka amesema katika kikao hicho pia, Kamati Kuu imempitisha Shekha Mpemba Faki kuwa Mgombea Ubunge wa Jimbo la Konde lililopo Kaskazini Pemba Visiwani Zanzibar katika uchaguzi mdogo utakaofanyika baadae mwaka huu.

Pia Chama hicho kimempongeza Rais Samia Suluhu Hassan na Rais wa Zanzibar, Dk Hussein Ali Mwinyi kwa namna ambavyo wanafanya kazi vizuri huku wakitekeleza ilani ya Chama Cha Mapinduzi ya mwaka 2020/25.
Share To:

Post A Comment: