Mwenyekiti wa Klabu ya Waandishi wa Habari Mkoani Tanga (Tanga Press Club) Lulu George akizungumza na waandishi wa habari

KLABU ya Waandishi wa Habari Mkoa wa Tanga imeandaa Bonanza ambalo litafanyika Jumamosi wiki hii kwenye uwanja wa shule ya Msingi Bombo Jijini Tanga.

Akizungumza na waandishi wa habari leo Mwenyekiti wa Klabu ya Waandishi wa Habari Mkoani Tanga (Tanga Press Club) Lulu George amesema kwamba bonanza hilo linalenga kuimarisha mahusiano baina ya waandishi wa habari na wadau.

Lulu alisema mbali na kuimarisha mahusiano kati ya waandishi na wadau pia linalenga kuwajenga waandisha wa habari kiafya pamoja na wadau kuiwezesha miili yao kuwa na kinga imara inayoweza kukabiliana na magonjwa mbalimbali.

“Hili ni bonanza la kwanza kwa mwaka huu tumeandaa na tutaendelea kuhakikisha tunayaandaa mara kwa mara kwa lengo la kuimarisha mahusiano mazuri na hii itasaidia kuweza kutekeleza vema shughuli zetu za kila siku na wadau”Alisema Lulu George

Mwenyekiti huyo aliwataka wadau mbalimbali wakiwemo wanahabari kushiriki kwa wingi ili kufanikisha zoezi hilo lenye manufaa ya kimahusiano na kiafya.

Awali akizungumza katika mkutano huo,Katibu wa Klabu ya Waandishi wa Habari mkoa wa Tanga Mbonea Herman alisema bonanza hilo litahusisha michezo mbalimbali ikiwemo Joging,Kuvuta kamba,Mpira wa miguu,kukimbiza kuku na kukimbia kwa kutumia gunia.

Mbonea alisema bonanza hilo litaanza kwa staili ya matembezi asubuhi yatakayoanzia kwenye viwanja vya Klabu wa Waandishi wa Habari iliyopo karibu na Polisi Mess na kuelekea katika viwanja vya shule ya Msingi Bombo mahali ambapo shughuli hiyo zitafanyika.

Tukio hilo ni la kwanza kufanyika katika kipindi cha mwaka huu 2021 lakini mpango katika mwaka huu ni kuwa na matukio mbalimbali ya kijamii ikiwemo kuendesha zoezi la uchangiaji wa damu baada ya kuonekana jambo hilo ni muhimu kwa jamii.


Share To:

TANGA RAHA BLOG

Post A Comment: