WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa ametoa siku saba kuanzia leo (Alhamisi, Desemba 17, 2020) kwa Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu, maofisa wanaochambua maombi ya ununuzi wa magari Ofisi ya Waziri Mkuu na wakurugenzi wa Jiji la Mwanza, Halmashauri ya wilaya ya Chato, Msalala na Kahama wajieleze kwa sababu gani magari hayo yalinunuliwa kwa gharama kubwa.

Ametoa agizo hilo leo (Alhamisi, Desemba 17, 2020) wakati akizungumza na watumishi wa umma, Waheshimiwa Wabunge, madiwani katika jiji la Mwanza na Manispaa za Ilemela na Nyamagana katika hoteli ya Malaika, jijini Mwanza. Amesema magari hayo ni mzigo kwa wananchi.

Waziri Mkuu amesema hayo ni matumizi mabaya ya fedha za umma na haiwezekani viongozi hao watumie magari ya gharama kubwa badala ya kutumia fedha hizo kwa ajili ya maendeleo ya wananchi na ametaka muongozo wa ununuzi wa magari uliotolewa na Serikali uzingatiwe.

Amesema matumizi ya fedha za umma lazima yasimamiwe ipasavyo na kwamba Serikali haina mzaha na mtumishi yeyote atakayebainika kutumia vibaya fedha za umma, hivyo amewataka madiwani wakasimamie vizuri maeneo yao.

Waziri Mkuu amewataka Wakurugenzi wahakikishe wanatoa ushauri ipasavyo katika Mabaraza ya Madiwani kuhusu matumizi na manunuzi, pia watoe kipaumbele katika udhibiti wa mapato na rasilimali za umma. “Wakurugenzi zingatieni vipaumbele vya wananchi na Halmashauri zetu katika kupanga matumizi na manunuzi na tumieni fedha za mapato ya ndani kutekeleza miradi ya kimkakati.”

Waziri Mkuu amewataka viongozi wa halmashauri waweke mikakati madhubuti itakayowezesha makusanyo ya Halmashauri zao yafikie asilimia 100 au zaidi. “Kuweni wabunifu wa vyanzo vipya vya mapato na ongezeni kasi ya ukusanyaji wa mapato kwenye Halmashauri zenu.”

Kadhalika, Waziri Mkuu amewataka watumishi wa umma wahakikishe wanawafuata wananchi hasa waishio maeneo ya vijijini walipo na kuwasikiliza kero zao na kushirikiana nao katika kuzipatia ufumbuzi

Wakati huo huo, Waziri Mkuu amerejea kauli yake aliyoitoa Desemba 7, 2020 ya kuwataka Makatibu Tawala wa Mikoa yote nchini wahakikishe kuwa watumishi wa idara nzima ya elimu hawaendi likizo mwisho wa mwaka huu, badala yake wakasimamie ukamilishaji wa ujenzi wa vyumba vya madarasa na madawati na wawe wamekamilisha ifikapo Februari 28, 2021.

“Watumishi wa idara ya Elimu Maafisa Elimu Wilaya na Mkoa, Wahandisi wa ujenzi, Maafisa Manunuzi wa Wilaya na Wakurugenzi wasipewe likizo kipindi hiki kuelekea sikukuu ya Krismasi na Mwaka mpya hadi Februari 28, 2020 ili wakamilishe ujenzi wa vyumba vya madarasa zaidi ya 3,000 kwa ajili ya wanafunzi wapya wa kidato cha kwanza ili waweze kuingia madarasani.

Kuhusu suala la kufanya ibada siku ya Krismas na Mwaka Mpya, Waziri Mkuu amesema watumishi hao hawajazuiwa kufanya ibada na badala yake watasali vituoni kwao na kwamba hajazuia watumishi hao kufanya ibada wakati wa sikukuu hizo.

Jumatatu, Desemba 7, 2020 Waziri Mkuu aliendesha kikao na Wakuu wa Mikoa, Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia na Katibu Mkuu Ofisi ya Rais-TAMISEMI kwa njia ya video akiwa ofisini kwake Mlimwa, jijini Dodoma na kupokea taarifa ya maandalizi ya mapokezi ya wanafunzi wa kidato cha kwanza, 2021.


(mwisho)
IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU

Share To:

Post A Comment: