Na. Elinipa Lupembe.
   Mkuu wa wilaya ya Arumeru Jerry Muro amewapiga marufuku, uwepo wa madalali wa kuuza mchanga maarufu kama 'Steringi', madalali ambao wanajipatia pesa nyingi bila kufanya kazi wala kulipa kodi za serikali na kuwanyonya wanaofanyakazi halali katika migodi ya mchanga Mirongoine.
     Marufuku hiyo, imetolewa baada ya wafanya biashara hao kuchoshwa na tabia za 'Masteringi' hao na kufikisha kero hiyo kwa mkuu huyo wa wilaya ya Arumeru,  na kulazimika kufanya mkutano wa pamoja, uliowakutanisha wafanyabiashara wa madini ya mchanga katika kijiji cha Mirongoine na Oljoro kata ya Oljoro wilaya ya Arumeru, uliofanyika kwenye ofisi ya kijiji cha Mirongoine.
    DC Muro amewataka Mastering hao kuacha mara moja, kufanyakazi ya udalali katika machimbo hayo, badala yake kutafuta kazi nyingine halali itakayowaingizia kipato, baada ya kukerwa na unyonyaji unaofanywa na Mastering hao dhidi kwa wamiliki wa migodi, wachimbaji, wapakiaji na wamiliki wa malori yanayopakia mchanga, kundi  ambalo hulipa kodi halali za serikali.
    Kwa pamoja wafanyabiashara hao, wamelalamikia kitendo cha 'Masteringi' hao kuwa miungu watu katika uendeshaji wa shughuli machimbo mgodini hapo, kwa kujipatia pesa nyingi ambazo hawazifanyii kazi wala kuzilipia kodi yoyote ya Serikali, jambo linalosababisha unyonyaji na  migogoro baina ya kundi la wafanya biashara wa eneo hilo.
    Wafanyabiashara hao, wameweka wazi kuwa, uwepo wa madalali 'Mastringi''' katika machimbo hayo, unasababisha migogoro na unyanyasaji, kwa kuwa bila Stering mwenye lori hawezi kununua mchanga, wala mmiliki wa migodi hawezi kuuza  mchanga mpaka amlipe 'Steringi' kiasi cha shilingi elfu 15 mpaka 20, kutegemea ukubwa wa gari, jambo linalosababisha  wafanyabiashara  kushindwa kufanya kazi hizo kwa amani pamoja na kuikosesha serikali mapato.
     "Inatukera sana 'Stering' mmoja anashikilia magari hata 10 kwa siku, na kujiingizia wastani wa shilingi laki moja na nusu mpaka mbili pesa ambayo, hajaitolewa jasho wala kuilipia kodi yoyote kwa serikali, wakati wamiliki wa malori na migodi hulipa kodi zote za serikali huku wapakiaji wa mchanga, wakiambulia shilingi elfu 2 mpaka 3 kwa kupakia mchanga kujaza lori.
     Hata hivyo Mkuu huyo wa wilaya, licha ya kusikitishwa na tabia ya 'Mastring' na  kupiga marufuku shughuli za 'Mastering' hao, kufanyakazi hizo katika machimbo hayo, amewataka vijana wanaopakia mchanga kuunda umoja wao muda huo,umoja utakaowawezesha kupata vibali vya kufanyakazi hiyo kihalali katika machimbo hayo.
    Frank Aberinego, Mwenyekiti wa Umoja wa wapakiji, amemshukuru Mkuu wa wilaya kwa kuwaondolea kero hiyo iliyodumu jwa miaka mingi sasa, na kuongeza kuwa, baada ya utatuzi wa kero hiyo wanategemea kufanya kazi kwa amani inayowawezesha kupata riziki na mapato ya serikali, kwa maendeleo ya taifa.

Mkuu wa wilayaya Arumeru Jerry Muro akizungumza na wafanya biashara wa kwenye migodi ya mchanga Mirongoine kata ya Oljoro, halamashauri ya Arusha, kwenye kikao kilichofanyika kwenye ofisi ya kijiji Mirongoine.  







Share To:

msumbanews

Post A Comment: