Naibu Waziri wa Afya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Dkt. Godwin Mollel wakati akizungumza na Menejimenti ya Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya na waandishi wa habari mjini Morogoro leo.
Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya Bw. Bernard Konga akielezea mikakati ya Mfuko katika kuwahudumia wanachama wake na kuwafikia wananchi wengi zaidi.
Mkurugenzi Mkuu wa Bohari ya Dawa Brig. Jen Dkt. Gabriel Sauli Mhidize akielezea mikakati ya upatikanaji wa dawa katika vituo.
Sehemu ya Menejimenti ya NHIF wakisikiliza maelekezo ya Serikali kupitia Naibu Waziri wa Afya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Dkt. Godwin Mollel.

Na Mwandishi Wetu, Morogoro

SERIKALI imezionya Hospitali zote nchini kuacha mara moja kufanya udanganyifu katika madai ya malipo yatokanayo na huduma wanazozitoa kwa wanachama wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya.

Hayo yamesema leo na Naibu Waziri wa Afya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Dkt. Godwin Mollel wakati akizungumza na waandishi wa habari mjini Morogoro kuhusiana na uboreshaji wa huduma za NHIF kwa wanachama na wananchi kwa ujumla.

“Serikali itaendelea kuulea Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya ili uimarike na kuendelea kupanua wigo na ubora wa huduma kwa wananchi wote, hivyo natoa onyo kwa vituo vinavyojihusisha na udhanganyifu wowote,” alisema Dkt. Mollel..

Alisema kuwa Serikali ya  Awamu ya Tano chini ya uongozi wa Mhe Rais Dkt. John Pombe Magufuli imeendelea kuweka mikakati mbalimbali ya kuboresha upatikanaji wa huduma bora za afya kwa wananchi ambapo mikakati hiyo ni pamoja na  pamoja na kuongeza bajeti ya dawa kutoka bilioni 30 mwaka 2015 hadi kufikia bilioni 270.

“Tumeona uboreshaji wa miundombinu ya huduma za Hospitali ikiwemo ujenzi wa Zahanati, Vituo vya Afya, Hospitali za Wilaya na Hospitali za Rufaa za Mkoa, kuongeza Madaktari katika vituo vya kutolea huduma za afya ngazi za chini na kuongeza vifaa tiba na vitendanishi ili kuwezesha wananchi wengi kupata huduma karibu na maeneo wanayoishi, haya ni mafanikio makubwa ambayo yameonekana” alisema Mhe. Naibu Waziri.

Alisema kuwa kutambua umuhimu wa Bima ya Afya kwa Wananchi na huduma zitolewazo na Bohari Kuu ya Dawa (MSD), Serikali kupitia Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto imekutana na Viongozi waandamizi wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya na MSD kwa lengo la kupanga mikakati ya utatuzi wa changamoto mbalimbali zinazojitokeza katika utekelezaji wa majukumu ya Taasisi hizo.

Kutokana na kikao hicho, Serikali imefanya maboresho katika orodha ya Taifa ya Dawa muhimu kwa kuongeza aina ya dawa 71 ambazo hazikuwepo awali ambapo Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya tayari umeongeza dawa hizo katika kitita chake cha mafao kitolewacho kwa wanufaika wake.

“Tumeuelekeza Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya kuwasilisha maboresho ya kitita cha huduma zitolewazo kwa wanachama kwa ajili ya maamuzi na kuanza kutumika; Kufanya mapitio ya utaratibu wa mikopo itolewayo kwa watoa huduma ikiwemo ya dawa, ukarabati wa vituo, vifaa tiba na vitendanishi ili kuongeza tija na kupunguza gharama,” alisema.

Katika hatua nyingine, Mhe. Naibu Waziri aliielekeza Menejimenti ya Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya kubuni na kutekeleza mikakati ya kuwawezesha wananchi wengi zaidi kujiunga na kunufaika na Mfuko huo ili kufikia adhma ya Serikali ya Afya Bora kwa wote na kuhakikisha inaharakisha utekelezaji wa kutambua huduma za kibingwa bobezi kama upasuaji wa moyo, tiba ya saratani na ubadilishaji viungo karibu na wananchi kwa kuanzia na Hospitali za Kanda.

Katika kikao hicho, Naibu Waziri huyo aliongozana na Mganga Mkuu wa Serikali Prof. Abel Makubi na Mkurugenzi Mkuu wa Bohari ya Dawa Brig. Jen Dkt. Gabriel Sauli Mhidize.
Share To:

msumbanews

Post A Comment: