Katibu Tawala Mkoa wa Shinyanga, Albert Msovela akizungumza wakati akifungua kikao cha uhamasishaji huduma za afya ya uzazi na mtoto leo Alhamis Julai 2,2020 kilichohudhuriwa na waganga wa tiba mbadala, watu maarufu,viongozi wa dini,viongozi wa Baraza la Wazee mkoa wa Shinyanga,Waandishi wa habari, Sekretariati ya mkoa,timu ya uendeshaji huduma za afya na Mwakilishi wa Wizara ya Afya Maendeleo ya Jamii,Jinsia, Wazee na Watoto, John Yuda kwa lengo la kukumbushana wajibu wao katika jamii inayowazunguka juu ya afya ya uzazi na mtoto mchanga.
Katibu Tawala Mkoa wa Shinyanga, Albert Msovela akifungua kikao cha uhamasishaji huduma za afya ya uzazi na mtoto leo Alhamis Julai 2,2020.
Afisa Pogramu kutoka Wizara ya Afya Maendeleo ya Jamii,Jinsia, Wazee na Watoto, Idara ya Kinga Kitengo cha Elimu ya Afya kwa umma, John Yuda akizungumza katika kikao cha uhamasishaji huduma za afya ya uzazi na mtoto ambapo alisema "Lengo la serikali ni kuhakikisha kuwa tunapunguza vifo vya mama na mtoto”.
Afisa Pogramu kutoka Wizara ya Afya Maendeleo ya Jamii,Jinsia, Wazee na Watoto, Idara ya Kinga Kitengo cha Elimu ya Afya kwa umma, John Yuda akizungumza katika kikao cha uhamasishaji huduma za afya ya uzazi na mtoto ambapo alisema 
“Huu ni mwendelezo wa Kampeni ya ‘Tuwavushe Salama’ inayowalenga wanawake na watoto kwani Corona imeathiri mikakati ya serikali katika kuwahudumia wananchi.
Kushoto ni Kaimu Mganga Mkuu Mkoa wa Shinyanga, Dkt. Nuru Mpuya akielezea umuhimu wa kuhamasisha wanawake wajawazito kuhudhuria Kliniki na kujifungulia katika vituo vya afya ili kupunguza vifo vya mama na mtoto. Wa kwanza kulia ni Afisa Pogramu kutoka Wizara ya Afya Maendeleo ya Jamii,Jinsia, Wazee na Watoto, Idara ya Kinga Kitengo cha Elimu ya Afya kwa umma, John Yuda akifuatiwa na Katibu Tawala Mkoa wa Shinyanga, Albert Msovela.
Afisa Maendeleo ya Jamii Mkoa wa Shinyanga Tedson Ngwale (kushoto) na Mratibu wa Elimu ya Huduma za afya mkoa wa Shinyanga, Halima Hamis wakiwa kwenye kikao cha uhamasishaji huduma za afya ya uzazi na mtoto.
Washiriki wa kikao cha uhamasishaji huduma za afya ya uzazi na mtoto mkoa wa Shinyanga wakiwa ukumbini.
Washiriki wa kikao cha uhamasishaji huduma za afya ya uzazi na mtoto mkoa wa Shinyanga wakiwa ukumbini.
Washiriki wa kikao cha uhamasishaji huduma za afya ya uzazi na mtoto mkoa wa Shinyanga wakiwa ukumbini.
Mratibu wa Elimu ya Huduma za afya mkoa wa Shinyanga, Halima Hamis akizungumza katika kikao cha uhamasishaji huduma za afya ya uzazi na mtoto na kuwataka wanawake wajawazito kuhudhuria kliniki na kujifungulia katika vituo vya afya ili kupunguza vifo vya mama na mtoto. Na Kadama Malunde - Shinyanga
Wawakilishi wa Makundi mbalimbali ya kijamii mkoa wa Shinyanga wamekutana katika kikao cha uhamasishaji huduma za afya ya uzazi na mtoto ili kuhamasisha matumizi huduma za afya ili kupunguza vifo vya mama na mtoto baada ya taifa kuathiriwa na Janga la ugonjwa wa homa kali ya mapafu (COVID -19) ambalo limejenga hofu kwa jamii na kusababisha kuzorota kwa matumizi ya huduma za afya.
Kikao hicho kimefanyika leo Alhamis Julai 2,2020 katika ukumbi wa ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga ambapo Mgeni rasmi alikuwa Katibu Tawala Mkoa wa Shinyanga, Albert Msovela.
Miongoni mwa washiriki wa kikao hicho ni Viongozi wa vyama vya watu wenye ulemavu,waganga wa tiba mbadala, watu maarufu,viongozi wa dini,viongozi wa Baraza la Wazee mkoa wa Shinyanga,Waandishi wa habari,sekretariati ya mkoa, timu ya uendeshaji huduma za afya na Mwakilishi wa Wizara ya Afya Maendeleo ya Jamii,Jinsia, Wazee na Watoto, John Yuda.
Akifungua kikao hicho, Katibu Tawala Mkoa wa Shinyanga, Albert Msovela alisema ugonjwa Corona ulijenga hofu kubwa kwa wananchi iliyopelekea kutopata huduma za afya kwa wakati likimo kundi la wajawazito na watoto.
Alieleza kuwa, takwimu za mkoa wa Shinyanga zinaonesha kuwa kwa mwaka 2019 kulikuwa na vifo 50 vitokanavyo na uzazi, mwaka 2018 vifo 56 na kuanzia mwezi Januari hadi Juni mwaka 2020 kuna vifo 15 vitokanavyo na uzazi na vifo 322 vya watoto wachanga.
“Hii ni idadi kubwa katika kipindi cha miezi sita,hivyo pamoja na changamoto ya ugonjwa wa Corona ambao unaendelea kupungua kwa kiasi kikubwa tunatakiwa kuimarisha huduma zetu kwa kuhimiza jamii hasa wajawazito na watoto kuwahi kupata huduma katika vituo vya kutolea huduma za afya kila mara ili kupunguza vifo hivi”,alisema.
“Naomba kila mmoja katika jamii atumie nafasi yake kuelimisha umuhimu wa wanawake kuendelea kufika katika vituo vya afya ikiwa ni pamoja kuhudhuria kliniki na kujifungulia katika vituo vya afya ili kupunguza vifo vitokanavyo na uzazi na watoto wachanga”.
“Maisha lazima yaendelee huku tukichukua tahadhari zote dhidi ya ugonjwa wa Corona kwa kuzingatia ushauri wa watalaamu wa afya na kila mmoja wetu atomize wajibu wake kulingana na nafasi yake katika jamii”,aliongeza Msovela.
Kwa upande wake Mratibu wa Elimu ya Huduma za afya mkoa wa Shinyanga, Halima Hamis alizitaja sababu zinazochangia vifo vinavyotokana na uzazi kuwa ni kutokwa damu nyingi kabla na baada ya kujifungua,kifafa cha mimba na kupasuka kwa mji wa mimba.
“Vifo hivi vinachangiwa pia na wajawazito kuchelewa kuanza kliniki chini ya wiki 12 na kutojifungulia katika vituo vya kutolea huduma huduma za afya. Hivyo ni vyema tukaendelea kuelimisha na kuhamasisha jamii juu ya kuwahi kliniki na kujifungulia katika vituo vya afya”,alisema Hamis.
Naye Afisa Pogramu kutoka Wizara ya Afya Maendeleo ya Jamii,Jinsia, Wazee na Watoto, Idara ya Kinga Kitengo cha Elimu ya Afya kwa umma, John Yuda alisema Wasimamizi wa jamii wakiwemo viongozi wa dini wana nafasi kubwa ya kuielimisha jamii kwa urahisi zaidi kutumia huduma za afya.
“Tumechagua kukutana na makundi haya kwa sababu ni makundi yanayoielewa jamii na yanasambaza elimu kwa haraka na rahisi zaidi kuliko hata wataalamu wa afya. Lengo la serikali ni kuhakikisha kuwa tunapunguza vifo vya mama na mtoto”,alisema Yuda.
“Huu ni mwendelezo wa Kampeni ya ‘Tuwavushe Salama’ inayowalenga wanawake na watoto kwani Corona imeathiri mikakati ya serikali katika kuwahudumia wananchi. Tunaendelea kusisitiza wanawake wajawazito kuhudhuria kwenye vituo vya afya”,alisema Yuda.
Kwa upande wao washiriki wa kikao waliahidi kwenda kutoa elimu na kuhamasisha jamii kuhusu umuhimu wa kuhudhuria katika vituo vya kutolea huduma za afya.
Share To:

Post A Comment: