Na Mathias Canal, Wizara ya Kilimo-Mwanza

Serikali imetangaza kwamba msimu wa ununuzi wa pamba wa mwaka 2020/2021 utazinduliwa tarehe 15 Juni 2020.

Waziri wa Kilimo Mhe Japhet Hasunga (Mb) ameyasema hayo leo tarehe 7 Juni 2020 wakati akizungumza kwenye mkutano maalumu wa wadau wa tasnia ya Pamba uliofanyika katika Ukumbi wa mikutano wa Chuo cha Benki kuu Jijini Mwanza.

Mhe Hasunga amebainisha kuwa msimu wa Pamba utazinduliwa wakati ambapo serikali imejiweka kando kutopanga bei elekezi katika zao hilo pamoja na mazao mengine badala yake bei za mazao zitatokana na soko.

Amesema kuwa kazi ya serikali ni kuhakikisha kuwa inasimamia uzalishaji bora wa mazao kadhalika kusimamia upatikanaji wa masoko ya mazao ili kuwa na bei nzuri yenye manufaa kwa wakulima.

Amesema kuwa kutokana na usimamizi madhubuti wa serikali kupitia Wizara ya Kilimo, uzalishaji wa pamba umeongezeka kutoka tani 122,178 msimu wa ununuzi wa 2015/2016 hadi tani 348,910 msimu wa 2019/2020.

Waziri Hasunga ameeleza kuwa zao la pamba ni mhimili wa uchumi wa wananchi wengi katika mikoa 17 na Wilaya 56 zinazozalisha zao hilo.

Kiwango   kikubwa cha uzalishaji kwa miaka ya karibuni kilifikiwa katika msimu wa ununuzi wa 2011/12 ambapo kiasi cha tani 357,133 za pamba zilizalishwa. Kutokea hapo, uzalishaji umekuwa ukishuka mwaka hadi mwaka ambapo katika msimu wa kilimo wa 2015/16 uzalishaji ulikuwa tani 122,178 kiasi ambacho ni kidogo kuwahi kuzalishwa nchini.
Amesema kuwa Serikali ya Awamu ya Tano chini ya Mhe Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ilipoingia madarakani, hatua kadhaa za makusudi zimechukuliwa na Wizara ya Kilimo ili kulinusuru zao la pamba ambapo malengo ya Wizara kwa sasa ni kuzalisha tani 1,000,000 za pamba ifikapo mwaka 2022/2023.
Amezitaja Hatua zilizochukuliwa na serikali kuwa ni pamoja na kuhamisha makao makuu ya Bodi ya Pamba kutoka Dar es Salaam kwenda Mwanza ili kuwa karibu na maeneo yanayolima pamba na kuwahudumia wakulima kwa karibu zaidi. Kutokana na hatua hiyo, ufanisi wa utendaji na huduma kwa wakulima umeongezeka.
Mfuko wa Wakfu wa Kuendeleza Zao la Pamba kurejeshwa Bodi ya Pamba ili kuimarisha usimamizi wa fedha zinazokusanywa na utoaji wa huduma kwa wakulima kwa lengo la kuboresha kilimo cha Pamba.
Hatua nyingine ni kuanzishwa kwa mfumo rasmi wa kuzalisha mbegu bora za kupanda. Kwa mara ya kwanza wakulima wote wa pamba kuanzia msimu wa kilimo wa 2018/19 wamepanda mbegu zilizothibitishwa (certified seeds). Aidha, mbegu mpya ya UKM08 yenye uwiano mkubwa wa pamba nyuzi wa asilimia 38-42 ukilinganisha na mbegu aina ya UK91 iliyokuwa na asilimia 32-35 ndiyo inayopandwa na wakulima. Kwa kuwa nyuzi zina thamani kubwa kuliko mbegu, UKM08 inampatia mkulima mapato makubwa zaidi kwa kuongeza bei anayolipwa.
Waziri Hasunga amesema kuwa mafanikio ya zao la Pamba yamechagizwa na kubadilisha mfumo wa upuliziaji wa viuadudu ili kukabiliana na mabadiliko ya tabianchiKuimarisha upatikanaji na usambazaji wa pembejeo kwa wakulima kwa kuwapatia mbegu bora za kupanda, viuadudu, vinyunyizi na molasisi pasipo kulipa fedha taslimu na wakulima kulipa pembejeo hizo kwa kukatwa shilingi 100 kwa kila kilo moja ya pamba katika mjengeko wa bei.
Kadhalika ni pamoja na kubadili mfumo wa ununuzi wa pamba kwa kuwaondoa mawakala wa kampuni binafsi na badala yake kutumia Vyama vya Ushirika vya Msingi (AMCOS). Kwa kuchukua hatua hii, ubora wa pamba umeongezeka kutoka asilimia 22 msimu ununuzi wa 2017/18 hadi asilimia 65 msimu wa 2019/2020. 
Kwa upande wake Naibu Waziri wa Kilimo Mhe Hussein Bashe (Mb) amesema kuwa msimu wa ununuzi wa zao la Pamba 2019/2020 haukuwa rahisi lakini kwa kiasi umekuwa na mafanikio makubwa ambapo amewashukuru wakuu wa Mikoa ya uzalishaji kwa usimamizi madhubuti wa zao la Pamba jambo lililopelekea kuongezeka kwa uzalishaji na tija. 
Pia amewapongeza wafanyabiashara/wanunuzi wa Pamba, Sekta mbalimbali za fedha zikiwemo Benki N.k kwa kushirikiana na serikali kuhakikisha kuwa pamba ya wakulima inanunuliwa. 
Ameongeza kuwa serikali iliamua kuwalipa wakulima wa Pamba kupitia Account zao za Benki hivyo jumla ya Account 128,000 za wakulima wa Pamba zimefunguliwa huku zoezi hilo likiendelea.
Naye Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara Mhandisi Stela Manyanya akitoa salamu za Wizara hiyo amesema kuwa wanunuzi/wafanyabiashara wanapaswa kujipanga zaidi baada ya serikali kutekeleza wajibu wake ili kuhakikisha kuwa msimu wa zao la Pamba utakapoanza wakulima waweze kupata bei nzuri na yenye tija. 

Share To:

Post A Comment: