Mbunge wa Dodoma Antony Mavunde akiwahutubia wananchi wake mtaa wa Gawaye
........................................................

Mbunge wa Jimbo la Dodoma Mjini Mh Anthony Mavunde amewahakikishia upatikanaji wa Nishati ya umeme kwa wananchi wote ambao bado hawajafikiwa na Nishati ya Umeme waliopo katika Jiji la Dodoma kufuatia utekelezaji wa program maalum ya usambazaji wa umeme utakaofanywa na TANESCO pamoja na REA mapema mwanzoni mwa mwaka 2020 katika maeneo 34 yaliyosalia.

Mbunge Mavunde ameyasema hayo leo kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika katika Mtaa wa Gawaye,Kata ya Chihanga ambao ulikuwa mahsusi kusikiliza kero za wananchi katika eneo hilo.

"Kufuatia maombi ambayo niliwasilisha Wizarani juu ya changamoto ya umeme katika baadhi ya maeneo ya Jiji La Dodoma,Waziri wa Nishati Dr.  Medrad Kalemani amewapa miezi 6 TANESCO kuanzia mwezi huu,kutekeleza mpango wa usambazaji wa Nishati ya umeme kwenye Jiji la Dodoma ambao utagharimu kiasi cha Tsh bilioni 50 hali itakayopelekea kutatua changamoto za maeneo yote ambayo bado hayana umeme na hivyo kuchochea shughuli za kiuchumi katika maeneo husika"Alisema Mavunde

Aidha Mbunge Mavunde pia ameahidi kuyatafutia ufumbuzi matatizo ya maji chumvi,Miundombinu ya Shamba la Zabibu na Barabara ya Hombolo Makuyu-Gawaye-Mayamaya.

Katika hali isiyo ya kawaida,Mbunge Mavunde aliwasikiliza wananchi hao kero na changamoto zao bila kuzuiwa na mvua kubwa iliyokuwa ikimnyeshea kwa muda wote wa mkutano.
Share To:

Francis Godwin Mzee wa matukiodaima

Post A Comment: