Na Ferdinand Shayo,Arusha.
Shirika lisilokua la kiserikali la Infoy limeendeleza juhudi zake katika kuwawezesha vijana wanaojishughulisha na uzalishaji na usindikaji wa   bidhaa za lishe ili waweze kutokomeza tatizo la udumavu nchini pamoja na kupunguza utegemezi.
Mratibu wa Shirika lisilokua la kiserikali la Infoy Laurent ,Sabuni alisema hayo  katika maonyesho ya bidhaa za lishe yaliyoandaliwa na shirika hilo kwa kushirikiana na shirika la kuhudumia viwanda vidogo la Sido mkoa wa Arusha  ,ambapo alisisitiza kuwa wazalishaji na wasindikaji wa bidhaa za lishe wanapaswa kushiriki kutatua matatizo ya lishe duni katika jamii na kuhakikisha kuwa wanazifikisha bidhaa hizo vijijini.
Sabuni alisema kuwa wamekua wakitoa mafunzo kwa wasindikaji wa bidhaa za lishe  juu ya namna bora ya kusindika na kuzifungasha ili ziweze kuwafikia wateja na kusaidia kupunguza tatizo la udumavu  linalowakabili watoto wengi licha ya uzalishaji wa nafaka ulioko.
Meneja wa Sido mkoa wa Arusha Nina Nchimbi aliwataka wasindikaji  watengeneza unga wenye virutubisho na viini lishe ili kukidhi afya ya mlaji   na kuhakikisha suala la viwango vya ubora  katika  bidhaa za lishe  wanazozalisha unazingatiwa.
Nina alisema kuwa Sido imefanya juhudi za kuwaunganisha wajasiriamali hao na taasisi za ubora ikiwemo TBS,TFDA ili bidhaa zao ziweze kuthibitishwa ubora na kupata masoko ya kitaifa na kimataifa.
Kwa upande wao Wasindikaji na Wajasiriamali wa bidhaa za lishe Dorice Assenga na Walter David  wameeleza kuwa wamekua wakitoa elimu juu ya umuhimu wa matumizi ya unga wa lishe kwa watoto wadogo na kuzipeleka bidhaa za maeneo ya pembezeni na vijijini ambako kuna hitaji kubwa la lishe ili kuwasaidia kinamama  wajawazito na watoto chini ya miaka mitano.
Mtaalamu wa Lishe Prisca Mwakalasi alisema kuwa mchango wa wadau wa lishe ni mkubwa kwani madhara ya udumavu huonekana hasa mtoto anapokua na kuwa mtu mzima inakua vigumu kufanya maamuzi sahihi kwani anakua amedumaa hadi akili hivyo masuala ya lishe kwa watoto na watu wazima yanapaswa yapewe kipaumbele kwani lishe ni kiini cha maendeleo.
Share To:

msumbanews

Post A Comment: