Wananchi wa Kata ya Makilawa wilayani Ikungi mkoani Singida wamesema wameanza kusafisha magodoro yao baada ya kupata maji kupitia mradi wa Tanjet.

Hayo yalibainishwa juzi na Katibu Mwenezi na Itikadi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Kata ya Makilawa Stuu Babu wakati akizungumza mbele ya Mbunge wao Eribariki Kingu alipofanya  ziara ya kutembelea kata hiyo na kuzungumza na wananchi kuhusu masuala mbalimbali ya maendeleo pamoja na kuwahamasisha kujitokeza kwa wingi kujiandika katika daftari la kudumu la mpiga kura na kuhakikisha CCM inapata ushindi kwenye chaguzi zake.

“Kwa kweli tunampongeza mbunge wetu kwa kazi kubwa anayoifanya katika jimbo letu kwani tangu kijiji chetu kianzishwe mwaka 2002 hatukuwahi kuwa na maji lakini amefanikisha kutuletea maji kupitia mradi wa Tanjet ambapo tumeweza kusafisha na magodoro yetu” alisema Babu.

Diwani wa Kata hiyo Shabani Hassan alisema katika kutekeleza ilani ya CCM, Mbunge huyo ameweza kuchangia zaidi ya sh.milioni 20 katika shughuli mbalimbali za maendeleo
 jambo ambalo halikuwa kufanywa na wabunge watangulizi wake.

Katika ziara hiyo aliyoifanya na kutembelea baadhi ya vitongoji katika Kata za Makilawa na Iglanson aliweza kukagua miradi ya ujenzi wa shule na kuahidi fedha za kukamilisha miradi hiyo.

Katika hatua nyingine Kingu aliahidi kutoa sh.milioni 1.5 kutoka katika mfuko wa jimbo kama motisha kwa walimu wawili pekee wa kujitolea wa Shule ya Msingi ya Ishingisha kwa moyo wa uzalendo wa kujitolea kufundisha shule hiyo tangu ikiwa haina wanafunzi na sasa inawanafunzi 192.
Share To:

Post A Comment: