WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amezindua rasmi zoezi la uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura na kuwahimiza vijana waliotimiza miaka 18 wajitokeze kwa wingi kujiandikisha.

“Nitoe rai kwa vijana wote wa Kitanzania waliotimiza umri wa miaka 18 au wale ambao watatimiza umri huo ifikapo Oktoba, 2020 wajitokeze kwa wingi na kujiandikisha katika Daftari la Kudumu la Wapiga Kura. Hawa ndio walengwa wakuu kwa sababu wanaingia kwa mara ya kwanza katika uchaguzi.”

“Ikumbukwe kwamba, bila kujiandikisha hawataweza kutumia haki yao ya msingi ya kuchagua viongozi wanaowataka. Hivyo, kujiandikisha kwao kutawahakikishia ushiriki wao katika uchaguzi wa viongozi,” amesema Waziri Mkuu.

Waziri Mkuu ametoa rai hiyo leo, (Alhamisi, Julai 18, 2019) wakati akizindua zoezi la uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura lililofanyika kwenye uwanja wa Mandela, Manispaa ya Moshi, mkoani Kilimanjaro.

Waziri Mkuu ambaye amewasili mkoani Kilimanjaro leo asubuhi kwa ziara ya kikazi za siku nne, ametumia fursa hiyo kuwasisitiza vijana na wale wanaorekebisha taarifa zao kwamba hakuna mtu atakayeruhusiwa kupiga kura katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2020 kama hajajiandikisha katika Daftari la Kudumu la Wapiga Kura ama hana kadi ya mpigakura.

Amesema zoezi hilo ambalo limeanza leo, linafanyika kwa mara ya kwanza tangu kumalizika kwa uchaguzi mkuu wa mwaka 2015. Amesema litafanyika nchi nzima na linatarajiwa kukamilika Machi, 2020.

“Watakaohusika awamu hii ni wapigakura waliotimiza miaka 18 hivi karibuni, wale watakaotimiza miaka 18 wakati wa Uchaguzi Mkuu Oktoba 2020, waliohama kata au Jimbo na kuhamia maeneo mengine ya kiuchaguzi, waliopoteza kadi au kadi zao kuharibika, wanaohitaji kurekebisha taarifa zao mfano majina ambayo hapo awali yalikuwa yamekosewa sambamba na kuwaondoa wapiga kura waliopoteza sifa kama vile kufariki,” amesema.



Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu ameziasa asasi za kiraia ambazo zimepewa vibali vya kutoa elimu ya mpigakura, zijiepushe na ushabiki wa kisiasa na badala yake zizingatie mwongozo wa elimu ya mpigakura uliotolewa na Tume ya Taifa ya Uchaguzi.

“Nimeambiwa, Tume imetoa vibali vya kutoa elimu ya mpigakura kwa baadhi ya Asasi za Kiraia. Rai yangu kwa asasi zilizopata vibali hivyo ni kuendelea kutoa elimu hiyo kwa wananchi kwa kuzingatia mwongozo wa uliotolewa na Tume ya Taifa ya Uchaguzi. Niendelee kuwaasa pia kutohusisha ushabiki na mijadala ya kisiasa muda wote mtakapokuwa mkitoa elimu hiyo,” amesema.

Amesema ana imani kuwa wananchi wakipata elimu kuhusu uboreshaji kama inavyoendelea kutolewa, basi watahamasika kutumia haki yao ya kikatiba ya kujiandikisha katika daftari hilo na hatimaye kushiriki katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2020.

Amesema zoezi la majaribio ya uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura katika Kata ya Kibuta katika Halmshauri ya Wilaya ya Kisarawe na Kata ya Kihonda katika Halmashauri ya Manispaa ya Wilaya ya Morogoro, lilifanyika kwa mafanikio makubwa.

Mapema, akitoa maelezo kuhusu zoezi hilo, Mwenyekiti wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi, Jaji Semistocles Kaijage, alisema katika zoezi la sasa, Tume itaendelea kutumia teknolojia ya kielektroniki yaBiometric (BVR) na imeandaa BVR kits 3,000.

Alisema kwa Tanzania Bara, Tume hiyo imeongeza vituo vya uandikishaji kutoka 36,549 vilivyotumika mwaka 2015 hadi kufikia 37,407; kutokana na zoezi la uhakiki wa vituo vya kuandikisha wapiga kura lililoendeshwa mwaka jana.

“Kutokana na hilo, vituo 6,208 vilibadilishwa majina, vituo 817 vimehamishwa kutoka mtaa mmoja au kijiji kimoja na kwenda kingine na vituo 19 vilihamishwa kutoka kata moja kwenda kata nyingine.”

“Kwa upande wa Zanzibar, vituo vya uandikishaji vimeongezeka kutoka 380 na kufikia 407. Kwa sasa kila kijiji au mtaa, utakuwa na kituo kimoja,” alisema.

Alisema vituo vya uandikishaji vitafunguliwa saa 2 asubuhi hadi saa 12 jioni na zoezi la uboreshaji litafanyika kwa siku saba kwa kila kituo cha kujiandikisha iwe ni Tanzania Bara au Zanzibar.
Share To:

msumbanews

Post A Comment: