Na Ferdinand Shayo,Arusha.

Kampuni ya Mbegu ya Seedco imekuja na mbegu bora za mahindi aina ya Tumbili 419 ambazo zinahimili mabadiliko ya tabia ya nchi  ambayo yamekua yakisababisha uhaba wa mvua katika maeneo mengi nchini hivyo kumsaidia mkulima kupata mavuno mengi licha ya mabadiliko hayo.


Akizungumza katika Maonyesho ya kilimo Teknolojia yaliyofanyika katika  Taasisi ya Utafiti wa Kilimo Tari Seliani ,Meneja Mauzo wa Kampuni ya Seedco, Daniel Ulimboka alisema kuwa kwa sasa wamefanya utafiti na kuja na mbegu bora ambazo zinahimili hali ya ukame licha ya uhaba wa mvua bado zinaleta mavuno ya kutosha kwa mkulima.


 "Tuna mbegu aina ya tumbili  419 ambayo inafanya vizuri sana hasa katika kipindi hiki ambacho hakuna mvua za kutosha wakulima bado wamekua wakipata mavuno  na kufurahia kilimo" Alisema Daniel


Kaimu Katibu Tawala wa Mkoa wa Arusha aliwataka watafiti kubuni teknolojia zinazoendana na mabadiliko ya tabia ya nchi ili wakulima waweze kupata mazao badala ya kupata hasara kutokana na mabadiliko hayo ambayo yamekua yakileta athari na kusababisha kushuka kwa uzalishaji.


Aidha aliwataka Wakulima kuondokana na kilimo cha mazoea ili waweze kufanya kilimo chenye tija na kuwaletea manufaa wakulima na taifa kwa ujumla

Mkurugenzi wa Baraza la Nafaka Afrika Mashariki  Gerald Masila alisema kuwa wanafanya juhudi za kuwaunganisha wakulima na masoko ili waweze kupata faida ya kilimo chao na kujikwamua kiuchumi.

Kwa upande wao wakulima waliofika katika maonyesho hayo Yasinta Pius na Leskar Mollel wameiomba wadau kuzifikisha teknolojia hizo maeneo ya vijijini ili ziweze kuwanufaisha wakulima.
Share To:

Post A Comment: