Katibu Mkuu wa CCM, Dk. Bashiru Ally, amekemea viongozi wenye uchu na mali za chama, akiagiza waondolewe ili kuepusha migogoro isiyokuwa na tija ndani ya chama hicho.

“Msiwavumilie hawa viongozi wenye uchu na mali za chama. Wafukuzeni wote. CCM haina uhaba wa wanachama na kila mwanachama ana haki ya kuongoza. Hizi tabia za kulindana na kukingiana vifua ndizo zilizotufikisha hapa,” alisema.

Bashiru ameyasema hayo katika mkutano wa wanachama wa Wilaya ya Ubungo, Dar es Salaam jana.

Dk. Bashiru alisema kuna taarifa za kuwepo migogoro ya viongozi kugombania mali za chama kama ilivyo katika Kata ya Sinza, hasa Sinza B, suala ambalo linatakiwa kushughulikiwa.

Aliwataka wanachama na viongozi kuhakikisha wanatunza mali za chama na kuzilinda, pia kufuata utaratibu mpya uliowekwa, ambao unahitaji malipo yote yatumie mfumo rasmi tofauti na ilivyokuwa zamani.

“Kuna baadhi ya viongozi wanavuruga mfumo, hawalipi kwa kutumia ‘control number’, bado wanaendelea kupokea fedha taslimu na kuzipangia matumizi kiholela. Wengine wanasema mabanda hayana watu kumbe yana watu, wanafanya kama mali yao, hawa hawavumiliki,” alisema.

Alieleza kuwa kwa sasa hawatarajii kupokea fedha kutoka kwa matajiri, na kwamba chama kitaendelea kutumia rasilimali na miradi yake kujipatia kipato kujiendesha.
Share To:

msumbanews

Post A Comment: