Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe. Ummy Mwalimu akizungumza wakati akifungua mkutano wa viongozi wa Hospitali za Rufaa za Mikoa unaofanyika katika ukumbi wa mikutano wa chuo cha Mipango Jijini Dodoma.


NA WAMJW-DOM

Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe. Ummy Mwalimu amewataka Waganga Wafawidhi wa Hospitali za Rufaa za Mikoa nchini kuhakikisha wanakua na vifaa vya muhimu vya kutolea huduma za afya kwa wagonjwa wanaofika Hospitalini kupata matibabu.

Waziri Ummy amesema hayo wakati akifungua mkutano wa viongozi wa Hospitali za Rufaa za Mikoa unaofanyika katika ukumbi wa mikutano wa chuo cha Mipango Jijini Dodoma.

Waziri Ummy amewataka Waganga Wafawidhi hao kubainisha aina ya vifaa vya matibabu vinavyotakiwa kupelekwa katika Hospitali zao ili kuhakikisha mgonjwa anapofika Hospitalini hakosi huduma wakati anapoenda kupata matibabu.

“Mganga Mfawidhi unatakiwa useme vifaa gani ukivipata utaboresha huduma, hatutaki mgonjwa afike Hospitali halafu akose huduma, boresha kwanza kupata vifaa vya msingi kabla ya vile vikubwa kama CT-Scan”. Amesema Waziri Ummy.

Aidha, Waziri Ummy amesema lengo la Wizara ya Afya chini ya Serikali ya awamu ya tano ni kuhakikisha huduma bora za afya zinatolewa ili mwananchi akifika katika Hospitali za Rufaa aseme kweli huduma zimeboreshwa.

“Lengo la Serikali ya awamu ya tano ni kuhakikisha kila Hospitali ya Rufaa inakua na huduma za kipaumbele 13 zikiwepo huduma za mama na mtoto ili kusaidia kupunguza vifo vitokanavyo na uzazi na magonjwa mengine ambayo yanaweza kutibiwa bila kumpa rufaa mgonjwa”. Ameongeza Waziri Ummy.

Kwa upande wake, Naibu waziri wa Afya, Maendeleo ya jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Faustine Ndugulile amewataka Waganga Wafawidhi wa Hospitali za Rufaa za mikoa kuhakikisha wanasimamia vizuri ukusanyaji wa mapato kwa kufunga mfumo utakaotumika kukusanya mapato na kuachana na makaratasi.

“Tuendelee kuboresha huduma za afya na kusimamia ubora wa huduma tunazozitoa na kuboresha upatikanaji wa vifaa na kuwa wabunifu japokuwa tuna changamoto za rasilimali watu ila huduma za kibingwa ziboreshwe ili kupunguza rufaa za nje”. Amesema Dkt. Ndugulile.

Naye Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya, Dkt. Zainab Chaula amewataka Waganga Wafawidhi hao kuhakikisha wanaripoti taarifa za maendeleo ya Hospitali na atakayeshindwa kufanya hivyo hataendelea na uongozi. Pia amewataka Waganga Wafawidhi hao kuwa na ushirikiano ili kufanya sekta ya afya kuwa ya mfano.

“Tuhakikishe tunaweka mifumo vizuri ya kutoa huduma kwa wahitaji kuanzia ngazi ya chini kwa kufuata miongozo na mikataba iliyotolewa, na tufanye kazi kwa ushirikiano bila kujali cheo au nafasi ya mtu”. Amesema Dkt. Chaula.

Pamoja na hayo katika Mkutano huo Waziri Ummy alizindua muongozo wa uendeshaji wa Hospitali za Rufaa za Mikoa pamoja na jarida la afya ya jamii toleo la kwanza.

MWISHO
Share To:

Post A Comment: