Mkurugenzi wa
Tanzanite One Faisal Juma.
Na Mashaka Mhando, Arusha.
CHAMA cha Wanunuzi na Wauzaji
wa Madini nchini (TAMIDA) na wachimbaji wadogo wa madini ya vito mkoa wa Arusha
na Manyara, wameipongeza bajeti ya serikali ya mwaka 2019/20 kwa kuondoa kodi
za mashine za kukata madini.
Mwenyekiti wa TAMIDA, Sammy Mollel
amesema bajeti ya mwaka 2019/20 imeondoa kilio cha muda mrefu cha wachimbaji na wauzaji wa madini nchini.
Mollel alisema kuondolewa kwa kodi za
mashine za kukata na kusanifu madini, kutaongeza ajira kwa vijana wengi lakini
kutaongeza mapato ya serikalini kwani madini mengi yatasanifiwa na kuongezwa
ubora hapa nchini.
Mkurugenzi wa kampuni ya Tanzanite
One na Tanzanite Forever Faisal Juma alisema uamuzi wa serikali kuondoa
kodi katika mashine za kukata madini ni faraja kwa sekta ya madini.
“kuondoa kodi katika mashine za
kukata madini, inamaana watanzania wengi wataanzisha viwanda vidogo vya
kusanifu madini”alisema.
Alisema viwanda hivyo, licha ya
kukata madini na kusanifu na kuondoa changamoto zilizokuwepo, pia kutawasaidia
vijana wengi kupata ajira ya moja kwa moja.
"Kwa kitendo hiki walichofanya
serikali kuondoa kodi, wametuongezea ufanisi kwa kiwango cha juu lakini pia
vijana wetu watapata ajira," alisema Juma ambaye ana mashine 30 za
kuchakata madini na ameajiri vijana wakutosha.
Juma pia alipongeza bajeti kwa
kuanzisha dawati la kusikiliza malalamiko ya wafanyabiashara wanapokuwa na
malalamiko ya kodi kwani sasa kutaongeza uwazi na uwajibikaji.
Alisema kulikuwa na shida TRA hasa
suala la malalamiko ya makadirio ya ulipaji wa kodi hivyo kuwepo kwa chombo
hicho kutaondoa ukiritimba na usumbufu wa ulipaji kodi za makadirio.
“kulikuwa na shida unakadiliwa kodi
hakuna sehemu ya kulalamika lakini pia hata TRA walikuwa hawawezi kushusha bila
kupata muafaka sasa kutakuwa na chombo cha tatu ambacho kitamaliza
migogoro”alisema.
Mkurugenzi huyo alimpongeza Rais kwa
kuonesha kwamba amekuwa na nia madhubuti ya kuwasaidia wafanyabiashara kwa
kuondoa mlolongo wa kodi zaidi ya 54 ambazo zilikuwa zikimnyonga mfanyabiashara
nchini.
Post A Comment: