Na EZEKIEL NASHON, DODOMA.
WAZIRI wa Elimu Sayansi na Teknolojia
Profesa Joyce Ndalichako, amesema serikali kupitia wizara ya elimu inaendelea
kuboresha miondombinu katika elimu, ili kuhakikisha inaboresha sekta ya elimu
hapa nchini.
Ameyasema hayo leo Jijini Dodoma katika maadhimisho ya wiki ya
elimu iliyoenda sambamba na kutoa tuzo kwa wanafunzi waliofanya vizuri katika
mitihani yao ya mwisho ya kumaliza elimu ya Msingi na Sekondari hapa
nchini tukio lililofanyika Shule ya sekondari ya wasichana Msalato.
Amesema serikali inafanya jitihada kubwa kuhakikisha inatoa
elimu bora, ikiwamo kukarabati shule kongwe pamoja na vyuo vya ngazi zote
sambamba na kuweka usimamizi thabiti katika vyuo ambayo vinazalisha walimu ili
kupata walimu bora.
“Sisi kama serikali tunafanya jitihada kubwa kuhakikisha elimu
yetu inapanda, tunahakikisha shule zote kongwe tunazikarabati angalau ziendane
na hadhi ili watoto wetu wanasoma katika mazingira mazuri tukiwa pia
tunasimamia kikamilifu vyuo vyetu vizalishe walimu ambao watatufikisha
tunapotaka” amesema.
Katika sekta ya elimu ya ufundi amesema serikali imetenga kiasi
cha bilioni ishirini na mbili(22) kujenga chuo cha veta katika mkoa wa Kagera
ili kuinua sekta ya elimu ya ufundi sambamba na kuvikarabati vyuo vya veta kote
nchini pamoja na kujenga vyuo vipya katika wilaya mbalimbali hapa
nchini ili kuinua elimu ya ufundi.
Katika elimu ya juu amesema serikali imeboresha vyuo vikuu vyote
na imejenga maktaba kubwa chuo kikuu cha Dar es saalam, yenye
uwezo wa kubeba wanafunzi wengi kwa wakati mmoja, pia imetenga zaidi
ya bilioni sita(6) kujenga hosteli katika chuo kikuu cha Mzumbe
itakayoondoa changamoto ya makazi kwa wanafunzi.
Amewataka wanafunzi kusoma kwa bidii na kuacha
uzembe, kwani serikali imekuwa ikifanya jitihada
kubwa katika kuboresha elimu, wao kama hawatafanya jitihada
kusoma itakuwa kazi bure.
“Niwaambie wanafunzi serikali hata ikijenga magorofa au kuleta
vitabu lori zima kama hamjitumi kusoma basi ni kazi bure ninashoowaomba ni
ninyi kujituma katika kusoma ili jitihada hizi za serikali ziweze kuzaa
matunda” amesema.
Kwa upande wake Mkurugenzi msaidizi wa idara ya elimu
kutoka TAMISEMI, Odilia Mushi, amevitaka vitengo vyote ya elimu
kutoka TAMISEMI kuhakikisha wanaimarisha malezi kwa watoto ili
waweze kupata matokeo mazuri.
Amesema tafiti mbalimbali zinaonyesha kuwa ufaulu
hapa nchini unaongezeka na umekuwa ukipanda mwaka baada ya mwaka na kuwataka
wasimamizi kuweka njia nzuri katika kuhakikisha ufaulu unaongezeka zaid.
Katika tuzo hizo zimetolewa kwa wanafunzi kumi (10) bora wa
shule za msingi waliofanya vizuri mitihani yao ya darasa la saba,
katika ngazi hiyo wanafunzi hao wamepewa vyeti na fedha kiasi cha laki
tano(500,000) kila mmoja.
Kwa upande wa kidato cha nne wanafunzi kumi bora katika
ngazi hiyo wametuzwa vyeti na fedha kiasi cha milioni
moja(1,000,000) kila mmoja, kwa ngazi ya kidato cha sita waliwekwa
katika makundi matatu na kuwa na idadi ya wanafunzi tisa(9) ambapo kila mmoja
ametuzwa vyeti na fedha taslimu milioni moja na laki tano(1,500,000).
Post A Comment: