Mkuu wa mkoa wa Rukwa Mh. Joachim Wangabo akikabidhi hundi kwa moja ya kikundi cha walemavu wa ngozi katika hafla fupi ya kukabidhi mikopo kwa vikundi vya wajasiliamali vya vijana, wanawake na watu wenye ulemavu iliyofanyika katika ukumbi wa manispaa ya Sumbawanga 28.6.2019

Mkuu wa mkoa wa Rukwa Mh. Joachim Wangabo akikabidhi hundi kwa moja ya kikundi cha walemavu wa ngozi katika hafla fupi ya kukabidhi mikopo kwa vikundi vya wajasiliamali vya vijana, wanawake na watu wenye ulemavu iliyofanyika katika ukumbi wa manispaa ya Sumbawanga 28.6.2019
Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Mh. Joachim Wangabo ameisifu Halmashauri ya Manispaa ya Sumbawanga kwa kuzidisha kiwango cha asilimia 10 ya mikopo kwa Vijana, akina Mama na Watu wenye Ulemavu kwa kutoa shilingi 253,228,000/= zaidi ya lengo la awali ambapo halmashauri ilitakiwa kutoa Shilingi 2,212,104,000/= kutokana na makisio ya makusanyo yake ya ndani yaliyolenga kukusanya Shilingi 2,212,104,000/=.
Mh. Wangabo alisema kuwa kiwango hicho cha asilimia 10 ambachoo Manispaa ya Sumbawanga wameweza kukitoa ni sawa na asilimia 115 kutokana na mapato yaliyokusanywa ya shilingi Bilioni 3.1 ambayo ni tofauti na makadirio yaliyofanyika kwa mwaka wa fedha 2018/2019.
“Taarifa ya Mkurugenzi imeonesha kuwa kuna mafanikio ya kujivunia katika suala zima la uwezeshaji Wananchi Kiuchumi kwa kipindi cha Miaka sita, kiwango cha fedha kinachotolewa kama mtaji kwa wajasiriamali kimekuwa kikiongezeka kila Mwaka na kwa Mwaka huu wa fedha 2018/2019 Manispaa imevunja rekodi kwa kutoa Shilingi 253, 228,000/= jambo hili ni la kupongezwa kwa mafanikio mliyofikia ya kutoa fedha 10% ya mapato ya ndani kwa 115% haya ni mafanikio makubwa sana, hivyo Hongereni sana Manispaa ya Sumbawanga,” Alisema.

Aidha, aliupongeza uongozi mzima wa Wilaya ya Sumbawanga pamoja na Halmashauri hiyo kwa kutekeleza sheria ya fedha ya mwaka 2018 inayoelekeza utekelezaji wa uwezeshaji wa vijana, kinamama na watu wenye ulemavu na kuzitaka halmashauri nyingine za mkoa kuiga mfano huo na hatimae kuwafaidisha wananchi kwa mikopo isiyo na riba ili waweze kujiinua kiuchumi.

Wakati akisoma taarifa ya utoaji wa mikopo Mkurugenzi wa manispaa ya Sumbawanga Jacob Mtalitinya alisema kuwa siku ya leo (28.6.2019) Halmashauri itatoa mikopo kwa vikundi 32 ambapo kati ya hivyo vikundi vya Wanawake 13, Vijana 14 na Watu wenye Ulemavu 5 ambapo kiasi cha Tsh. 73,678,000 kitatolewa kama uwezeshaji wa Wananchi.
“Kwa maana hiyo, Halmashauri ya Manispaa ya Sumbawanga kwa kipindi cha mwaka 2018/19 itakuwa imeweza kutoa mikopo kwa vikundi 114 vikiwemo vya Wanawake 56, Vijana 44 na watu wenye ulemavu 14 Ambapo kiasi cha jumla ya Tshs. 253,228,000.00 zitakuwa zimetolewa kwa makundi yaliyoainishwa. Hivyo itapelekea kufikiwa kwa jumla ya wanachama 1,135 kama wanufaika wa mikopo hiyo kwa mwaka wa fedha 2018/2019,” Alieleza.
Pamoja na mafanikio hayo makubwa, Mtalitinya hakusita kugusia changamoto ambazo halmashauri inakumbana nazo ikiwemo Hamasa ndogo ya uanzishwaji wa vikundi vya kiuchumi, Uelewa mdogo wa Jamii kuhusu uanzishwaji wa vikundi vya kiuchumi, Uelewa mdogo wa fursa za kiuchumi kwa Jamii. Kukosekana kwa masoko ya bidhaa za vikundi. Na hivyo kuahdi kuendela kutoa elimu  ya ujasiriamali kwa vikundi  ngazi ya kata na mitaa.
Katika hatua nyingine Mh. Wangabo alichukua fursa hiyo kukabidi kikombe cha ushindi wa jumla wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa kwa mwaka 2018 ambapo Halmashauri ya Manispaa ya Sumbawanga iliibuka na ushindi huo. 
Share To:

Post A Comment: