Na.WAMJW,Dodoma

Tanzania imeazimia kufikia asilimia sabini kutoka arobaini na nane ya uhaba wa watoa huduma za afya kwa nchi za Afrika Mashariki na Kusini mwa Afrika ifikapo mwaka 2022.

Hayo yamesemwa leo na Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Ummy Mwalimu wakati akifungua kikao cha kujadili changamoto za rasilimali watu katika sekta ya afya kati ya viongozi kutoka  Wizara ya Afya, Tamisemi pamoja na washirika wa maendeleo nchini.

Waziri Ummy amesema lengo la kikao hicho ni kujadili changamoto  mbalimbali zinazohusu rasilimali watu ikiwemo ya upungufu wa  watumishi, ajira, mafunzo pamoja na mahitaji ya watumishi kuanzia ngazi za zahanati hadi hospitali za wilaya nchini.

Amesema upungufu huo umetokana na ongezeko la miundombinu ambayo imewekwa na serikali ya awamu ya tano licha ya kazi kubwa iliyofanyika ya kuimarisha upatikanaji wa dawa na vifaa tiba.

”ingawa  bado ipo changamoto  ya rasilimali watu  katika sehemu za kutoa huduma za afya nchini  ambapo pengo ni takribani asilimia 52 kwa kila watumishi wa afya  mia moja  tunawahitaji watumishi arobaini na mbili”. Amesisitiza Waziri Ummy.

Aidha, etaja sababu nyingine ya upungufu wa watumishi wa sekta ya afya kuwa ni pamoja na ongezeko la magonjwa yasiyo ya kuambukiza hivyo inahitajika watoa huduma wa afya wengi katika kuwahudumia wananchi wenye matatizo hayo.

Hata hivyo Waziri Ummy amesema kikao hicho kitaweka mikakati ya pamoja na ya ubunifu ya kuona kunakuwa na maboresho ya uzalishaji wa wataalam wa afya na wale wanaozalishwa ni kiasi gani wanaweza kuajiriwa na kuwekwa kwenye utumishi wa umma hususan kwenye ngazi ya zahanati na hospitali za wilaya.

“Tutaweka ubunifu ambao utawawezesha mfano wauguzi kupatiwa mafunzo ya kutoa dawa za usingizi na hii ni kuona wanao uwezo wa kufanya kazi nyingine tofauti, kwa ujumla sekta ya afya nchini inaenda vizuri na nina amini kwa pamoja tunaweza kutatua uhaba wa watumishi katika sekta ya afya.

-Mwisho-
Share To:

msumbanews

Post A Comment: