Mnamo Mei 04, 2019 majira kati ya saa 19:00 na 20:00 usiku huko Vwawa, Wilaya ya Mbozi na Mkoa wa Songwe, Mtu mmoja aitwaye MDUDE MPALUKE NYAGALI [31] ilibainika kuwa amechukuliwa na watu ambao hakuweza kuwatambua na kupelekwa mahali pasipojulikana.

Taarifa zilifikishwa Polisi Mkoa wa Songwe na ufuatiliaji ulianza mara moja na mnamo tarehe 08 Mei, 2019 majira ya saa 21:00 usiku huko Inyala katika Kijiji cha Mtakuja kilichopo Mkoa wa Mbeya alionekana mtu anaomba msaada, ndipo Dereva wa Pikipiki @ Bodaboda aitwaye EMMANUEL KANAMGONDE na mwenzake AYUB WILSON walimbeba na Pikipiki hadi kwa uongozi wa serikali wa Kijiji cha Mtakuja.

Mhanga wa tukio hili baada ya kufikishwa kwa viongozi wa Kijiji hicho alijitambulisha kuwa yeye anaitwa MDUDE MPALUKE NYAGALI wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo na akaomba wajulishwe viongozi wake. Kisha Mhanga alipelekwa Hospitali ya Rufaa Kanda ya Mbeya kwa uchunguzi zaidi wa kitabibu.

Upelelezi wa shauri hili unaendelea ikiwa ni pamoja na msako mkali wa kuwatafuta waliohusika katika tukio hili.
Share To:

msumbanews

Post A Comment: