WAZIRI MKUU, Kassim Majaliwa ameutaka uongozi wa Benki ya CRDB uzidi kuzingatia misingi ya utawala bora na kuongeza juhudi katika utoaji wa huduma ili benki hiyo iendelee kuwa mfano wa mafanikio kwa taasisi zinazomilikiwa nakuendeshwa na wazalendo.

Ameyasema hayo leo (Ijumaa, Mei 17, 2019) wakati akifungua semina ya wanahisa wa benki ya CRDB katika Ukumbi wa Mikutano wa Kimataifa wa Arusha (AICC) jijini Arusha. Semina hiyo inahudhuriwa na wanahisa 1,500.

Amesema Serikali ya Awamu ya Tano inayoongozwa na Rais Dkt. John Magufuli imeendelea kuimarisha misingi ya utawala bora ili kuleta matokeochanya, hivyo ni vema kwa uongozi wa benki hiyo ukaizingatia. 

“Serikali imeendelea kuhakikisha kwamba katika utekelezaji wa shughuli mbalimbali kunakuwepo na uwazi, uwajibikaji, ushirikishaji wa watu, ufanisi, tija, uadilifu, usawa, kuzingatia taratibu za kisheria, kanuni na miongozo inayotolewa na Viongozi wakuu wa kitaifa.” 

Waziri Mkuu amesema Serikali imeendelea kusisitiza misingi hiyo ya utawala bora ili kujiridhisha kuwa taasisi mbalimbali zikiwemo za kifedha zinaongozwa kwa kufuata misingi hiyo. 

“Serikali imeendelea kusisitiza uwazi katikakuendesha shughuli za umma na makampuni yanayomilikiwa nawananchi bila usiri na kificho. Lengo ni kuwapa wananchi uwezo wakupima utendaji na uzingatiaji wa kanuni, taratibu na sheria.”

Waziri Mkuu amesema lengo la Serikali ni kuhakikisha wananchi wa jinsia zote na makundi yote wanahusishwa katika kupanga nakufanya maamuzi ya mambo yanayowahusu ili kuwawezesha kujiletea maendeleo. 

“Nyote ni mashahidi kuwa Serikali imeendelea kuhimiza utendaji unaozalisha matokeo  yanayokidhi lengo na matarajio ya watu na kuhakikisha taasisi za kifedha zinatimiza ndoto za wananchi katika kupata huduma nzuri ikiwemo upatikanaji wa mikopo na elimu ya matumizi bora ya fedha.”

Hivyo, Waziri Mkuu amesema ni vema benki hiyo kupitia kitengo chake cha elimu ihakikishe inatoa elimu kwa umma juu ya matumizi mazuri ya fedha zikiwemo za mikopo ili wananchi waweze kuitumia vizuri na kujiongezea tija.

Awali, Mkurugenzi Mtendaji wa benki ya CRDB, Abdulmajid Msekela alisema zaidi ya asilimia 80 ya hisa za benki hiyo zinamilikiwa na Watanzania ikiwemo Serikali, hivyo uongozi wa benki hiyo una jukumu kubwa la kuhakikisha wanatoa huduma bora.

Alisema wamejipanga kuboresha huduma zao ili wanahisa waweze kujivunia uwekezaji wao walioufanya kwenye benki hiyo. “Tupo tayari kuhakikisha benki ya CRDB inasonga mbele zaidi ikiwa ni pamoja na kuboresha huduma kwa wateja.”

Mkurugenzi huyo alisema kuwa mbali na kuboresha huduma kwa wateja, pia wataongeza ufanisi katika utoaji wa huduma na hatimaye waweze kutoa gawio kubwa kwa wanahisa wao. 

Kwa upande wake,Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Charles Kicheere ambaye alimuwakilisha Waziri wa Fedha na Mipango katika semina hiyo, alitumia fursa hiyo kuwashauri wananchi wajenge tabia ya kuwekeza kwenye hisa. Alisema mwamko wa  Watanzania katika kuwekeza kwenye hisa bado ni mdogo.
Share To:

msumbanews

Post A Comment: