Rais  Magufuli amesema alipokuwa mdogo alitamani kuwa Askofu lakini hajui ni nini kilitokea akashindwa kuingia katika njia hiyo.

Akizungumza katika ibada ya kuzindua Jimbo Kuu la Kanisa Katoliki Mbeya na kumsimika Askofu Mkuu, Gervas Nyaisonga, Rais Magufuli amesema anashanga hadi sasa pamoja na matamanio yake hayo ameshindwa kuwa hata Katekista au Mwenyekiti wa jumuiya.

“Nilitamani sana kuwa Askofu lakini sijui ni nini kilitokea nikashindwa kuwa hata Katekista lakini au hata mwenyekiti wa Jumuiya.

“Leo nimefurahi na ninawaonea wivu Maaskofu, nilitamani niwe huko lakini niko huku, mlioko huko msitoke ni pazuri, sasa hivi niko huku na bado natamani kuja huko,” amesema Rais Magufuli.

Rais Magufuli pia aliwakumbusha Maaskofu kuhusu wito wa kazi ya uaskofu kupitia Kitabu cha Biblia cha 1Timotheo 3:1 unaosema “Ni neno la kuaminiwa mtu akitaka kazi ya Askofu atamani kazi njema.”

Kwa upande wake Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki Dar es Salaam, Polycarp Kadinali Pengo, amelitaka Kanisa kutimiza wajibu wake wa kuwasimamia waumini kiroho bila kusahau kutoa ushirikiano kwa serikali katika kuweka mazinga mazuri ya kiutawala.

“Tunahitaji uwepo wa roho mtakatifu katika kuboresha mazingira ya waumini ambao wanatambua vyema wajibu wao katika kuwaongoza vyema waumini, serikali ndiyo inayoweza kulifanya hili katika upeo mpana wa kiutawala, ili roho mtakatifu aweze kutenda kazi tunahitaji kuwa na kanisa linaloshirikiana vyema na serikali,” amesema Kadinali Pengo.
Share To:

msumbanews

Post A Comment: