Na Idara ya Habari-NEC
Mwili wa aliyekuwa Mtumishi wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) na Mwandishi wa Habari mkongwe Bwana CLARENCE SABAYA NANYARO umeagwa jijini Dar es salaam na nyumbani kwake Kongowe-Kibaha mkoani Pwani leo Ijumaa tarehe 05 April, 2019.
Mwili wa marehemu umesafirishwa kwenda Kijiji cha Nkoamara Wilaya ya Arumeru Mkoani Arusha kwa mazishi yanayotarajiwa kufanyika kesho jumamosi April 06.
Ibada ya kumuaga Marehemu Clarence Sabaya Nanyaro aliyefariki dunia Siku ya Jumanne April 03, mwaka huu  katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili alikokuwa amelazwa kwa matibabu imefanyika mapema leo asubuhi katika kanisa la Kilutheri lililopo Hospitalini hapo na kuhudhuriwa na watu mbalimbali wakiwemo wanatasnia ya Habari.
Akiwasilisha salamu kwa niaba ya Uongozi na Wafanyakazi wa Tume Mkurugenzi wa Idara ya Habari na Elimu ya Mpiga Kura katika Tume ya Taifa ya Uchaguzi Bi. Giveness Aswile amemwelezea Marehemu kuwa alikuwa mfanyakazi aliyeitumikia taasisi yake kwa kujitoa kwa hali na mali pamoja na kujiwekea mipango kadhaa ya kuendeleza taasisi na Taifa kwa ujumla.
Nanyaro ambaye alikuwa Kaimu Mkuu wa Sehemu ya Habari katika Idara ya Habari ya Tume ya Taifa ya Uchaguzi pia alikuwa akiendelea na masomo ya Shahada ya Uzamivu katika Mawasiliano ya Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustino kampass ya Dar es salaam.
Miongoni mwa taasisi alizofanya kazi wakati wa uhai wake ni pamoja na Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC), Ofisi ya Makamu wa Rais, Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi na Tume ya Taifa ya Uchaguzi ambako alifanya kazi hadi mauti yalipomkuta.
Marehemu Clarence Sabaya Nanyaro ambaye alizaliwa April 01 Mwaka 1969 huko katika Kijiji cha Nkoamara Wilayani Arumeru mkoa wa Arusha ameacha mke na watoto wanne (4).
Mwisho    
Share To:

Post A Comment: