Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Joyce Ndalichako amewaagiza wanafunzi wanaosoma masomo ya Sayansi na wabunifu nchini kubuni vitu ambavyo vitasaidia kurahisisha shughuli mbalimbali.

Amesema hayo jana Alhamisi Machi 7, katika kilele cha Mashindano ya Sayansi, Teknolojia na Ubunifu  (MAKISATU) jijini Dodoma ambayo kauli mbiu yake ni ‘kukuza ujuzi na ubunifu kwa uchumi wa viwanda’ ambapo amesisitiza wananchi kujitokeza kwa wingi kuonyesha ubunifu wao ili kukuza uchumi wa nchi.

“Changamoto tuliyonayo kwa sasa ni muamko kwa wananchi haujafikia katika kiwango ambacho serikali ingependa kukiona, ni wazi kabisa tunapaswa kuwa na ubunifu na kutumia sayansi na teknolojia kuhakikisha tunarahisisha maisha ya wananchi wanaoishi vijijini.

“Ninatoa wito kwa wabunifu wote nchini kuhakikisha wanajikita kuangalia ni kwa namna gani wanarahisisha shughuli zinazofanyika katika mazingira yao na ikumbukwe ubunifu hauna umri na hauchagui kwasababu mwisho wa siku mkono unaenda kinywani,” alisema.

Aidha Ndalichako alisema washindi waliopatikana katika mashindano hayo wataendelezwa ili waweze kukuza tafiti zao kwa lengo la kukuza uchumi.

Kwa upande wake Kaimu Katibu Mkuu Profesa James Mdoe alisema  lengo la Mashindano hayo yaliyohusisha wabunifu kutoka ngazi mbali za Elimu ni kuibua ubunifu, umahiri, kuchochea ugunduzi kwa lengo la kukuza matumizi ya Sayansi na Teknolojia katika maendeleo.

Mashindano hayo  yalifunguliwa rasmi na Naibu Waziri Mhe. William Ole Nasha Machi 5, 2019 na jana yamefikia kilele ambapo washindi mbalimbali walipata zawadi za fedha na kutunukiwa vyeti.
Share To:

msumbanews

Post A Comment: