Aliyekuwa Mbunge wa Arumeru Mashariki, Joshua Nassari amesema atakwenda mahakamani kutafuta haki ya uwakilishi wa Wananchi wa Arumeru baada ya Spika wa Bunge, Job Ndugai kutangaza kwamba hana sifa za kuendelea na ubunge.

Nassari ameyasema hayo wakati akizungumza na waandishi wa habari Leo na kusema kuwa mara ya mwisho alihudhuria mkutano wa Bunge wa Septemba lakini hakuhudhuria mkutano wa Novemba na Januari kwa sababu alikuwa anamuuguza mke wake huko Marekani.

"Nilifanya jitihada za kuwasiliana na Spika, nikamtumia ‘email’ (barua pepe) nikiwa Marekani kumjulisha hali ya mke wangu, Nasikitika kwa uamuzi alioufanya nawapa pole wananchi wangu wa Arumeru, haki yao tutaitafuta kwenye vyombo vya sheria," amesema Nassari.

Akizungumza kwa huzuni Nassari amesimulia jinsi alivyokuwa akimuuguza mke wake kutokana na matatizo aliyokuwa nayo na kusema alijaaliwa kupata mtoto wa kike Januari 27, siku moja kabla ya kuanza kwa mkutano wa Bunge la Januari.

Amesema alikuwa njia panda kuamua kati ya kuhudhuria vikao vya Bunge au kukaa na mke wake ambaye alikuwa mgonjwa, ambapo amekiri kuwa hajutii uamuzi wake wa kusimamia kiapo chake cha ndoa kwa kuamua kumuuguza mke wake.

"Pamoja na huzuni ya kuvuliwa ubunge, bado nina furaha ya kupata mtoto, kwani kuwa mbunge hakuondoi majukumu mengine ya kifamilia. Spika alihudhuria harusi yangu mwaka 2014, alikuwa anajua sina mtoto na nilimjulisha juu ya matatizo ya mke wangu. Alitakiwa kujiridhisha kwa kuniita na kunihoji badala ya uamuzi alioufanya," ameongeza Nassari.

Kwa mujibu wa  taarifa ya Bunge iliyotolewa Machi 14 ilieleza kwamba Nassari alikosa sifa za kuwa mbunge kwa kutohudhuria mikutano mitatu mfululizo ya Septemba, Novemba na Januari.
Share To:

Post A Comment: