Waziri wa Elimu Sayansi na Teknolojia Profesa , Joyce Ndalichako amesema  serikali iko tayari kuendelea kutoa ushirikiano katika Taasisi binafsi ambazo zimeendelea kutoa mchango mkubwa katika sekta ya Elimu hapa nchini.

Waziri Ndalichako amesema hayo mkoani Dodoma wakati akizindua jengo la shule ya Msingi Misercodia inayomilikiwa na kanisa katoliki Shirika la Watawa wa Misericordia.

Waziri Ndalichako amesema Serikali imekuwa ikitambua na kuheshimu kazi kubwa inayofanywa na kanisa hilo katika kusaidia ujenzi wa miundombinu kwenye sekta ya Afya na Elimu hapa nchini na ikiwa ni pamoja na  kutatua changamoto mbalimbali kwa wakati.

"Wakati nakuja kuzindua shule hii  nilimtaarifu Mheshimiwa Rais Dkt. John Magufuli na ametuma salamu, amesema niwaambie anawashukuru sana Maaskofu na Watawa kwa kuwa  mnaunga mkono juhudi za Serikali katika  ushiriki wa miradi mbalimbali ya maendelea kwa vitendo,”amesema Waziri Ndalichako.

Waziri huyo wa Elimu amesema , ujenzi wa Miundombinu hiyo umekuja wakati muafaka ambapo uhitaji wa shule za mchepuo wa kingereza ni mkubwa , kutokana na watumishi wengi wa serikali kuhamia Dodoma na hivyo kuhitaji shule kwa ajili ya watoto wao.

Kuhusu malezi ya wazazi, Waziri amesema hivi sasa wazazi wamesahau majukumu yao na badala yake wamekuwa wakifanya kazi zote ambazo zilipaswa kufanywa na watoto jambo ambalo sio sawa kwani wanajenga taifa la wavivu.

Waziri Ndalichako pia amezipongeza shule  nyingine za dini kwa kusimamia maadili kwa wanafunzi, ambapo ametumia  nafasi hiyo kuwakaribisha wawekezaji kuja kuwekeza kwa kujenga miundombinu ya shule za msingi na sekondari kwani hivi sasa Dodoma inauhitaji mkubwa wa shule kwa sasa.

Waziri Ndalichako ameipongeza shule kwa kufanya vizuri katika matokeo ya kidato Cha Nne na Sita na kuongoza kitaifa katika somo la kiingereza, pia amezipongeza shule nyingine za dini kwa kusimamia maadili kwa wanafunzi.


Imetolewa na:
Kitengo Cha Mawasiliano Serikalini
WIZARA YA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA
8/9/2018
Share To:

msumbanews

Post A Comment: