Mwimbaji wa Kwaya ya Vijana ya Kanisa la AICT Chang’ombe (CVC), Mariam Charles (22) amekutwa amefariki katika nyumba ya wageni iliyopo Buza anakodaiwa alikuwa na mchumba wake (jina linahifadhiwa kwa sasa).


Kwa mujibu wa baba mzazi wa marehemu, Charles Lutonja, mwanaume huyo ambaye pia ni mwimbaji wa kwaya hiyo inayotamba na albamu ya ‘Pazia la Hekalu’, tayari alishatoa posa kwa Mariam Aprili mwaka huu na alikuja jijini Dar es salaam kwa ajili ya kutoa mahari.

Akisimulia tukio hilo, Lutonja alisema mchumba wa Mariam alimpigia simu mama wa marehemu, Jumatatu ya Septemba 3 na kumueleza kuwa anakuja jijini Dar es Salaam kwa ajili ya kutoa mahari leo Ijumaa.


“Basi mke wangu aliniambia lakini nilishangaa mbona ni ghafla hata hivyo tulikubali,” alisema.


Alisema Jumanne, Septemba 4, mara baada ya kijana huyo kuwasili jijini Dar es Salaam akitokea Dodoma, Mariam aliaga anakwenda kuonana naye katika nyumba ya wageni aliyofikia.


“Aliondoka nyumbani saa 8 mchana, akamuaga mama yake (Ester) kuwa anakwenda kuonana na mchumba wake, lakini jioni alituma ujumbe kuwa atachelewa,” alisema.


Lutonja alisimulia zaidi kuwa usiku huo (Jumanne) hakurudi na ilipofika juzi asubuhi (Jumatano) mama yake Mariam alipokea ujumbe kutoka kwa kijana huyo uliosema: “Mwanao tayari nimemuua.”


Alisema baada ya hapo walianza kumtafuta Mariam na waliporipoti kituo cha polisi Chang’ombe walipewa saa 24 za kusubiri iwapo kuna taarifa zozote.


“Lakini jana (Jumatano), tulienda kituoni tena na tukaambiwa kuna mwili umeletwa umekutwa gesti, tulipoukagua tukagundua ni wa Mariam,” alisema.


Alisema kijana huyo, hakutuma ujumbe huo kwa mama wa marehemu tu, bali alituma pia kwa wanakwaya wengi wa Vijana (CVC) akiwaambia kuwa wanamchonganisha na Mariam.


“Baada ya kutuma huo ujumbe, tulijaribu kupiga simu hiyo lakini haikupatikana na taarifa zote hizi zipo polisi,” alisema. Kwa mujibu wa Lutonja, mwili wa Mariam unaonyesha amenyongwa.


Mariam alikuwa anajishughulisha na biashara ndogondogo huku akihudumu katika kwaya kama mwimbaji. Alikuwa ni mtoto wa sita wa Mzee Lutonja na sasa mwili wake umehifadhiwa katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili (MNH).


Hata hivyo Jeshi la Polisi Mkoa wa Temeke limechukua sampuli kutoka kwenye mwili wa Mariam na kupeleka kwa Mkemia Mkuu wa Serikali kwa ajili ya uchunguzi wa chanzo cha kifo hicho.


“Leo (jana) polisi wametuambia kwamba wamechukua sampuli kutoka kwenye mwili wa marehemu na kupeleka ofisi ya Mkemia Mkuu kwa ajili ya vipimo zaidi. Tumeruhusiwa kuendelea na mazishi na sisi tumeamua kuzika Jumamosi katika makaburi ya Temeke,” alisema Lutonja.


Alipoulizwa kuhusu tukio hilo, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Temeke, Emmanuel Lukula alikiri kuwa na taarifa na kwamba jeshi la polisi linaendelea na uchunguzi wake. Alisema wanashirikiana na Ofisi ya Mkemia Mkuu katika uchunguzi huo.


“Uchunguzi ni jambo pana na linafanyika kwa namna mbalimbali, kwa hiyo siwezi kusema mazingira ya kifo mpaka uchunguzi huo utakapokamilika, ndiyo maana tunachunguza,” alisema kamanda huyo alipoulizwa kuhusu mazingira ya kifo cha msichana huyo.


Akitoa maoni yake kuhusu tukio hilo, Rais wa Mtandao wa Wasanii wa Injili na Maadili ya Utaifa (Tagoane), Dk Godwin Maimu alisema kuna haja ya kutolewa kwa elimu ya urafiki, uchumba na ndoa makanisani ili kuwaepusha vijana na matukio hayo.


Alisema inasikitisha kwa watu wanaomwimbia Mungu kukutwa kwenye maeneo yasiyo ya kimaadili hasa kwa mtoto wa kike. Aliongeza kwa sasa ni wakati wa kuwapa mafunzo ya maadili ili watende yanayowapasa kutenda. “Vyama vya muziki nchini vitoe elimu makanisani juu ya urafiki, uchumba na ndoa. Vijana wakiwa na elimu ya masomo hayo, hawatakumbana na matatizo kama yaliyotokea kwa msichana huyo.”

MAMA AFUNGUKA 


Mama mzazi wa mwimbaji wa Kwaya ya Vijana ya Kanisa la AICT Chang'ombe (CVC), Mariam Charles (22), Ester Charles amesimulia kwa uchungu namna alivyopata taarifa za binti yake kuuawa siku chache kabla ya kulipiwa mahari.

Mwili wa Mariam ulikutwa katika nyumba ya kulala wageni ya 'East London’ iliyopo Buza anakodaiwa alikuwa na mchumba wake.


Akizungumza na MCL  mama huyo amesema Septemba 4 mwanae alimuaga kuwa anaenda kanisani kwenye kwaya.


“Baadaye akaniambia ameitwa na mchumba wake hivyo anaenda kuonana naye. Sikuwa na wasiwasi kwa sababu ni mchumba wake na binti alikuwa akiaga popote anapoenda," amesema.

Amesema baadaye alishangaa kupata ujumbe kutoka kwa mchumba wa mtoto wake unaosema; “Tayari nimemuua mwanao.”

"Nilishtuka na ikabidi tuanze kumtafuta Mariam na tukaenda polisi. Kusema kweli tangu hapo hali yangu nikawa sielewi hadi tulipokuja kuona kweli amemuua," amesema na kuongeza;

"Binti yangu alikuwa mpole, mnyenyekevu, hana ugomvi na mtu na aliniaga kila anakoenda.”

Dada wa Mariam, Pendo Lutonya amesema amesikitishwa na kifo cha kinyama cha mdogo wake kwa sababu badala ya kupokea mahari kama ilivyodaiwa, ameuawa.

"Mara ya mwisho nilikutana naye kanisani wiki iliyopita na alikuwa anaenda Morogoro kwenye huduma, sijamuona tena hadi leo mdogo wangu ameuawa," amesema.

Chanzo- Mwananchi
Share To:

Anonymous

Post A Comment: