Vigogo watatu wa zamani wa Chama Kikuu cha Ushirika, Mkoa wa Kagera KCU 1990 LTD wamesomewa mashitaka matano likiwamo la uhujumu uchumi na kusababisha hasara ya milioni 124.

Wakili Mwandamizi wa Serikali Athuman Matuma aliieleza mahakama ya Hakimu mkazi Mkoa wa Kagera jana kuwa watuhumiwa hao walitenda makosa hayo kwa nyakati tofauti mwaka 2011.

Washitakiwa hao ni Mwenyekiti wa zamani wa Bodi ya KCU, John Binunshu, aliyekuwa Meneja Mkuu KCU, Vedastus Ngaiza na aliyekuwa mhasibu, Bestina Rwebangira.

Aliyataja mashtaka hayo kuwa ni kula njama matumizi mabaya ya ofisi, kughushi, matumizi mabaya ya madaraka na kuhujumu uchumi kwa kuisababishia serikali hasara ya Sh124 milioni.

Watuhumiwa walisomewa mashtaka hayo mbele ya Hakimu Mkazi Mfawidhi John Kapokolo  na wamenyimwa dhamana hadi Jumatatu kesi yao itakapotajwa tena.
Share To:

msumbanews

Post A Comment: