Jeshi la Polisi limefungua jalada la uchunguzi dhidi ya kauli zilizotolewa na mbunge wa Kigoma Mjini (ACT-Wazalendo), Zitto Kabwe.

Akizungumza leo Jumatano Agosti Mosi, 2018 msemaji wa polisi, Barnabas Mwakalukwa amesema kwa sasa uchunguzi unafanyika kuhusiana na tuhuma zinazomkabili mbunge huyo ambaye pia ni kiongozi wa ACT.

Mwakalukwa ameeleza hayo ikiwa imepita siku moja tangu Waziri wa Mambo ya Ndani,  Kangi Lugola kumtaka kiongozi huyo kujisalimisha polisi  kwa maelezo kuwa ametoa kauli za uchochezi.

Lugola amesema Zitto ametoa kauli za uchochezi na kuwatukana viongozi wa Serikali wakati akizungumza katika mkutano wa hadhara uliofanyika katika jimbo la Kilwa Kusini, mkoani Lindi.

Katika mkutano huo Zitto alialikwa na mbunge wa jimbo hilo, Seleman Bungara maarufu Bwege.

Mwakalukwa amesema kufuatia agizo hilo la Lugola tayari wamefungua jadala kuchunguza jambo hilo, kwamba uchunguzi ukikamilika na iwapo itaonekana mbunge huyo anahitajika, watamuita polisi.

Amesema polisi wanafanya kazi kwa mujibu wa taratibu na sheria, kwamba Zitto akihitajika ataripoti kwa kamanda wa polisi mkoani Lindi.

Jana, Zitto alijibu kauli ya Lugola ya kumtaka aripoti polisi akibainisha kuwa atakwenda ikiwa atapewa wito wa kisheria.

Kupitia ukurasa wake wa mtandao wa kijamii wa Twitter Zitto amesema, “waziri hana hayo mamlaka. Kama polisi wananitaka watoe wito wa kisheria nitakwenda.”

“Naendelea na kampeni za ubunge wa Buyungu ambapo tunamuunga mgombea wa Chadema na madiwani wa ACT- Wazalendo kwenye kata kadhaa. Nashauri waziri ampate kwanza yule mbwa wa polisi bandari.“
Share To:

msumbanews

Post A Comment: