WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa ameongoza waombolezaji katika kuuaga mwili wa aliyekuwa mbunge wa Korogwe Vijijini, Bw. Stephen Ngonyani maafufu Profesa Maji Marefu.

Bw. Ngonyani ambaye alifariki dunia Julai 2, 2018 katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbi ameagwa leo (Jumatano, Julai 4, 2018) katika Viwanja vya Karimjee Jijini Dar es Salaam.

Waziri Mkuu ametumia fursa hiyo kutoa pole kwa wanafamilia, wabunge, wananchi wa Korogwe pamoja na Watanzania kwa ujumla. Amewataka waendelee kumuombea marehemu.

“Natoa pole kwa wake wa marehemu, watoto na nawaomba tuendelee kuwa wavumilivu na watulivu katika kipindi hiki. Tulimpenda sana lakini Mwenyezi Mungu amempenda zaidi,”.

Kwa upande wake, Katibu wa Bunge, Bw, Stephen Kagaigai akisoma wasifu wa marehemu amesema Bw. Ngonyani alizaliwa Mei 25, 1956 katika wilaya ya Songea mkoani Ruvuma.

Bw. Kagaigai amesema marehemu alianza kuugua Juni 17 mwaka huu na Juni 18 alilazwa katika Hopitali ya Mkoa wa Dodoma na Juni 20 alihamishiwa katika Hopitali ya Muhimbili.

Shughuli hiyo ilihudhuriwa na Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi John Kijazi. Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Dkt. Bashiru Ally, Spika wa Bunge, Bw. Job Ndugai, Naibu Spika Dkt. Tulia Ackson, Wabunge na wanafamilia.
Share To:

msumbanews

Post A Comment: