Mkurugenzi wa Halmashauri ya Arusha Dc Dkt. Wilson Mahera akimpa maelekezo Muwekezaji  Robert Daniel.

Wananchi wa Kijiji cha Losinoni juu kata ya Oldonyowasi Wilayani Arumeru Mkoani Arusha wamemuomba Rais Magufuli kumfutia hati Mwekezaji Robert Daniel Raia wa Uholanzi anayemiliki shamba la KORFOVOUNI lenye hekari 776.

Wakitoa malalamiko yao mbele ya Mkurugenzi wa Halmashauri Dkt.Wilson Mahera Pamoja na Mbunge wa Viti Maalum Mh. Amina Mollel wamedai kuwa Mwekezaji huyo anamiliki shamba hilo tokea mwaka 1940 ambapo sehemu kubwa ya zaidi ya hekari 410  ni milima yenye mawe ambapo mpaka sasa ameweza kumudu hekari 15 kati ya hekari 776 kwa kulima kilimo cha Kisasa cha Maua ( Green House).

Hata hivyo wananchi hao wameeleza kuwa walipomfuata kuomba ardhi kwa ajili ya maendeleo ya kilimo aliamua kuwakodishia wanakijiji hao hekari 255 kwa kulipa elfu Arobaini  ( 40000 ) kwa kila hekari moja kila wanapolima na bila kuwapa risiti huku akiwalazimisha wanakijiji hao kupanda miti mingi Mara tu wanapokodishiwa shamba hilo.

Sambamba na hapo wameeleza kuwa eneo hilo halina  mawasiliano mazuri ya Simu kero kubwa walioko nayo ni kwamba yanapokuja
Makampuni ya Simu ili yaweze kuwekeza minara kwenye milima hiyo inawabidi kupata kibali toka kwa muwekezaji huyo anayejipambambanua kumiliki milima hiyo.


Mmoja ya Mwananchi hao ameeleza kuwa mwaka 2015 waliamua kuandamana kutaka ardhi hiyo ili kuiendeleza ndipo alipotoa Hekari tatu tu kwa Ajili ya Ujenzi wa Shule.

Dkt. Mahera alipojaribu kumuuliza Mwekezaji huyo mbele ya wananchi kwanini anawakodishia ardhi badala ya kulima bure alimjibu mkurugenzi kuwa
"Wananchi ndio waliniomba kulipia kwa kila heka wanayokodishiwa "

Walipoulizwa wananchi hao na Mkurugenzi walidai kuwa bila hivyo wasingepewa Ardhi wakati walikuwa wanauhitaji wa mashamba ya kulima.

Mwekezaji huyo alipoombwa na Mkurugenzi kurejesha Baadhi ya Ardhi hiyo inayolimika ambayo hajaiendeleza kwa miaka kumi Alisema 
"Sipo tayari kuachia ardhi hii na nipo tayari kurudishwa kwetu kama italazimika."

Dr. Mahera amemtaka Mwekezaji huyo na wawekezaji wengine katika Halmashauri ya Arusha Dc ambao wanamiliki maeneo makubwa na kuyaita mashamba huku eneo wanalotumia kwa kuwekeza ni dogo na wakati huo akikodishia wananchi wayaendeleze kinyume chake itapendekezwa katika Wizara wapunguziwe ardhi hiyo ikizingatiwa kuwa Halmashauri hii haina ardhi kabisa.

Hata hivyo Mkurugenzi amewaasa wananchi hao kuchagua viongozi wanaowajibika kwa maslahi ya waliowachagua  huku akimuagiza Mwenyekiti wa Kijiji hicho kuhakikisha anampelekea Ofisini kwake Orodha na mikataba ya wanakijiji wote walioingia na muwekezaji huyo katika kulima ili kufuatilia Utekelezaji.
Share To:

msumbanews

Post A Comment: