Mwenyekiti wa Bodi ya Baraza la Michezo Tanzania (BMT), Leodegar Tenga ameliomba Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF)  liache kukurupuka na badala yake lipitie kwa kina sheria ya wachezaji 10 wa kigeni katika timu za Ligi Kuu.

Sheria hiyo iliyopitishwa hivi karibuni na TFF, inaruhusu timu zinazoshiriki Ligi Kuu nchini kusajili wachezaji wa kigeni 10 kutoka idadi ya awali iliyoruhusu timu inayoshiriki ligi kuu kuwa na wachezaji wakigeni saba.

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana  Jumatano Julai 25, Tenga alisema sheria hii ikiwezekana ipitiwe tena kwa kina ili ionekane kama inaweza kusaidia ligi hiyo.

“Kuwe na tathimini ya kina juu ya sheria hii tujiulize kama kweli inaweza kusaidia timu zetu na wachezaji wa hapa nyumbani pia tutafakari kama tunaweza kufika tunapokwenda kwa sheria hii.

“Wakati mwingine kuwa na ushirikishwaji mzuri ili watu watoe maoni yao juu ya hili jambo na hata tunaposajili wachezaji hawa tuhakikishe tunasajili wachezaji wenye viwango vizuri,” alisema Tenga.

Aidha, katika mkutano huo mwenyekiti huyo amesisitiza vyama vya michezo kitaifa kuhakikisha vinafuata sheria za kimichezo vizuri na kuhakikisha kunakua hakuna migogoro ya muda mrefu  kwenye vyama.
Share To:

msumbanews

Post A Comment: