Maelfu ya watalii kutoka sehemu mbalimbali duniani wanatembelea Hifadhi ya Taifa ya Tarangire iliyo umbali wa kilometa 118  kutoka jiji la arusha katika barababra ya lami ya Arusha-Dodoma, na Kusini Mashariki mwa Ziwa Manyara.

Jina la hifadhi hii yenye ukubwa wa kilomita za mraba 2,850 lina asili ya Mto Tarangire unaotiririsha maji mwaka mzima kuelekea upande wa Kaskazini mwa hifadhi hii ndio umeipa hifadhii hii jina hilo, sababu ya uwepo wake katika kipindi chote cha mwaka ni msaada mkubwa kwa maisha ya
wanyamapori ndani na nje ya hifadhii hii.

Hifadhi hii ni maarufu kwa makundi makubwa ya tembo wakubwa na wenye pembe ndefu kuliko hifadhi nyingine nchini Tanzania.


Pia inaongoza duniani kwa kuwa na tembo wengi kwenye eneo la kilometa za mraba, ambapo unaweza kuona kundi la tembo zaidi ya mia tano kwa mara moja. Hifadhi hii pia ina mandhari nzuri ya kuvutia inayotokana na maumbile ya mibuyu inayosadikiwa kuwa na umri wa zaidi ya miaka elfu nane.

Wanyama wa aina nyingi wanaopatikana ndani ya hifadhi hii ni pamoja na punda milia, nyumbu, swala, simba, nyati, kongoni, chui, duma na wengine wengi pamoja na aina 550 za ndege . Hifadhi hii ni maarufu katika ukanda wa kaskazini mwa Tanzania ambapo wengi, kutoka ndani na nje ya nchi kwani hupenda kutembelea hifadhi hii.

Umaarufu mwingine wa hifadhi hii ni pamoja ya aina ya chatu walio na uwezo wa kukwea miti. Kutokana na umaarufu huu idadi ya wageni wanaotembelea hifadhi imekuwa ikiongezeka mwaka hadi mwaka.

 Unaweza kutembelea hifadhi hii wakati wote wa mwaka na kuwaona wanyama wote bila matatizo kutokana na mazingira mazuri ya hifadhi yanayosaidiwa na Mto Tarangire unaokatiza katikati ya hifadhi.

Hifadhi ya Taifa ya Tarangire ina zaidi ya jamii 550 za ndege ambao ndio wamejulikana, na kati ya ndege hao baadhi yao wapo katika tishio la kutoweka. Tafiti zinaonyesha kwamba kipindi cha mvua ndio kipindi kizuri sana kwa aina nyingi za ndege kwenye eneo hili kuzaliana kwa wingi. Mabwawa na mito iliyopo katika hifadhi hii yanakuwa ndio sehemu nzuri zaidi ya kuona ndege wengi sana. Vile vile uoto wa asili katika hifadhi hii ndio unaopelekea wingi wa ndege katika eneo hili.

Tayari idadi ya watalii imeongezeka maradufu baada ya uongozi wa Shirika la Hifadhi za Taifa (TANAPA) kutangaza kikamilifu vivutio adimu, vilivyoko katika hifadhi hiyo.

Watalii wanaoongoza kila mwaka kutembelea hifadhi hiyo ni watalii wa nje, wakati watalii wa ndani ni wachache, hali inayotokana na ukweli kwamba Watanzania wengi kutojua kikamilifu vivutio vya hifadhi zao, hivyo hawajui wanachokikosa.

Takwimu za kuongezeka kwa idadi ya watalii Tarangire  zimo katika taarifa maalumu ya hali ya utalii katika Hifadhi ya Tarangire, iliyotolewa na Mhifadhi Mkuu wa Hifadhi ya Tarangire, Stephano Qolli.

 Kwa mujibu wa taarifa hiyo, idadi ya watalii wa ndani waliotembelea hifadhi hiyo mwaka 2008/2009 ilifikia 72,757 huku wale wa ndani ni 31,953, ambapo jumla ni watalii 104,710.
 Mwaka 2009/2010 watalii wa nje walikuwa ni 69,690 wakati watalii wa ndani walikuwa 33,136 na kufanya jumla ya watalii kuwa 102,826.

Taarifa inasema mwaka 2011/2012 watalii kutoka nje walikuwa ni 107,591 huku watalii wa ndani 47,795 hivyo kufikisha watalii 150,386.

 Mwaka jana jumla ya watalii 112,163 kutoka nje ya nchi, walitembelea hifadhi hiyo huku wale wa ndani 65,038, hivyo kufikisha watalii 177,201.
Share To:

msumbanews

Post A Comment: