Mwenyekiti wa Chama cha United Democratic (UDP), John Cheyo ameipongeza Serikali ya Awamu ya Tano kwa kununua ndege pamoja na kutekeleza miradi ya maendeleo ukiwemo ujenzi wa reli ya kisasa.

Wakati Cheyo akisema utekelezaji wa miradi hiyo unadhihirisha kuwa fedha ipo serikalini, mwenyekiti wa chama cha Tanzania Labour (TLP), Augustine Mrema amesema ununuzi huo wa ndege umeitoa Tanzania aibu ya kutokuwa na ndege licha ya wingi wa rasilimali.

Wametoa kauli hizo leo Jumapili Julai 8, 2018 katika hafla fupi ya mapokezi ya ndege mpya ya Serikali aina ya Boeing 787-8 Dreamliner inayowasili leo nchini.

“Rais ametuvisha nguo tulikuwa uchi. Tulikuwa hatuna ndege kubwa wakati tuna rasilimali nyingi. Sasa jina la Tanzania litatukuka dunia nzima," amesema.

Mrema ambaye aliwania urais mwaka 1995 kwa tiketi ya chama hicho na kushika nafasi ya pili, amewataka wananchi kuacha kumsema vibaya Rais Magufuli ili aweze kuchapa kazi.
Share To:

msumbanews

Post A Comment: