Baada ya basi la abiria  la Dar Express linalofanya safari zake Arusha - Dar es salaam kuteketea kwa moto  maeneo ya Tegeta,  Mkuu wa Kikosi cha Usalama Barabarani Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Marison Mwakyoma amesema bado wanamsaka dereva wa basi hilo ili kuweza kutoa maelezo ya kina juu ya ajali hiyo.

Kamanda Mwakyoma amesema kwamba ingawa taarifa za awali zinadai kwamba ni kufeli kwa breki ya nyuma, lakini zipo sababu za msingi ambazo zinaweza kutolewa na dereva huyo kwani tukio lililopelekea gari hilo kulipuka halikuwa la ghafla.

Akizungumzia ajali hiyo iliyotokea Tegeta  usiku wa kuamkia jana, Kamanda Mwakyoma amesema kwamba basi hilo lilitokea Arusha likuwa na abiria 42, ambapo 22 walishukia Bagamoyo na wengine waliosalia walifikia maamuzi  ya kushuka baada ya kuona gari linazidi kutoa harufu na ndipo dereva alipoamua kulitelekeza.

Aidha Mwakyoma ameongeza kwamba siyo kila ajali husababishwa na uzembe wa dereva kwani yapo mambo mengi ikiwepo nyaya za umeme kugusana, ku-jam kwa breki ya gari hivyo wamiliki wa magari wanapaswa kuwa makini wanapofanya 'service' ya magari ikiwa ni pamoja na kutazama mfumo mzima wa umeme na siyo kumwaga 'oil'.

Pamoja na hayo Mwakyoma amesema uchunguzi wa kina wa kuhusu ajali hiyo bado unaendelea kufanyika na sasa wanasubiria hati ya ukaguzi wa gari hilo kutokea Arusha kabla ya safari.
Share To:

msumbanews

Post A Comment: