RAIS Mstaafu, Dk. Jakaya Kikwete, amewataka waandaaji wa maonesho ya biashara ya kimataifa maarufu kama Sabasaba kuendelee kuwa wabunifu zaidi ili kuwezesha wajasiriamali kupata masoko ndani na nje ya nchi.

Kikwete aliyasema hayo jana alipotembelea baadhi ya mabanda ya biashara uwanjani hapo huku akigeuka kuwa kivutio kikubwa katika maonesho ya 42 ya biashara ya kimataifa yanayofanyika jijini Dar es Salaam baada ya wananchi waliofika katika maonesho hayo kufuata msafara wake.

Akizungumza baada ya kutembelea mabanda mbalimbali, Kikwete aliitaka Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kuwasaidia wafanyabiashara kutafuta masoko ya bidhaa wanazozalisha.

Kikwete alisema ameona bidhaa zote zinazotengenezwa na wafanyabiashara, hivyo kuna haja kubwa ya serikali kuwatafutia masoko wafanyabishara hao katika masoko ya kimataifa.

“Naona kila mwaka bidhaa zinaongezeka ubora wake ni vyema kuwatafutia masoko ili wakue zaidi,” alisema Dk Kikwete.

“Bidhaa nimeziona zinauzika ndani na nje ya nchi kazi kwenu wizara na Tantrade kuwasaidia wajasiriamali hawa ili wakue zaidi,” alisema Kikwete.

Kikwete aliingia katika viwanja hivyo saa 6:00 mchana na kupokewa na Naibu Waziri wa Viwanda Biashara na Uwekezaji, Mhandisi Stella Manyanya.

Baada ya kuingia katika uwanja  wa maonesho wananchi waliokuwapo katika viwanja hivyo waliacha shughuli zao na kumfuatilia nyuma huku wengine wakitaka kumpa mkono kumsalimia.

Katika ziara hiyo ya kutembelea mabanda, Kikwete aliongozana na Manyanya na Mkurugenzi wa Mamlaka ya Maendeleo ya Biashara (Tantrade), Edwin Rutageluka.
Share To:

msumbanews

Post A Comment: